1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Mahakama Uganda yafuta hukumu ya miaka 20 kwa Wakenya 32

Tatu Karema
25 Aprili 2024

Nchini Uganda mahakama ya kijeshi imeamuru kuachiwa huru kwa raia 32 wa Kenya waliokuwa wamehukumiwa kifungo cha miaka 20 kila mmoja gerezani mwaka jana 2023.

https://p.dw.com/p/4fBz5
Mahakama ya kijeshi yawaachia huru Wakenya 32 wakiwemo watoto
Mahakama ya kijeshi yawaachia huru Wakenya 32 wakiwemo watotoPicha: Hajarah Nalwadda/AP Photo/picture alliance

Watu hao kutoka jamii ya wafugaji wa kuhamahama ya Turkana walipatikana na hatia ya kuwa na silaha na risasi kinyume na sheria na kwa kila kosa walifungwa miaka kumi gerezani.

Ila mawakili wa watu hao waliwasilisha rufaa katika mahakama kuu ya jeshi wakitoa hoja kadhaa kwamba watu hao walikamatwa wakashtakiwa na kuhukumiwa katika muda wa siku moja tu bila kuwakilishwa na mwanasheria yeyote. Hii ilikuwa baada ya wao kukiri makosa hayo.

 

Aidha, sita kati ya washtakiwa walikuwa watoto chini ya umri wa miaka 18 na hawakustahili kufungwa na watu wazima pamoja na kwamba adhabu iliyotolewa kwao ilikuwa kali sana.

Jaribio la mwendesha mashatka la kutaka kesi dhidi yao iendeshwe upya limepingwa vikali na mawakili wakisema kuwa ni kinyume na katiba ya Uganda kuendesha kesi ambayo hukumu yake ilikwisha tolewa na mahakama nyingine.

Hii leo mamlaka ya magereza ilitarajiwa kuwakabidhi watu hao kwa jamaa zao ambao wamekuwa Uganda wakifuatilia kesi hiyo.