1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahkama Kuu Libya yathibitisha hukumu ya kifo kwa wauguzi wa kigeni.

Mohamed Dahman11 Julai 2007

Mahkama Kuu ya Libya leo imeshikilia hukumu ya adhabu ya kifo dhidi ya wanamatibabu sita wa kigeni kwa kuwambukiza watoto wa Libya virusi vya HIV lakini imefahamika kwamba adhabu hiyo inaweza kubadilishwa.

https://p.dw.com/p/CHB4
Kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi akabiliwa na kizungumkuti cha kesi ya wauguzi wa Bulgaria.
Kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi akabiliwa na kizungumkuti cha kesi ya wauguzi wa Bulgaria.Picha: AP

Mzozo huo wa Libya unafungaminisha haki za binaadamu na suala la kisiasa.

Waziri wa mambo ya nje wa Libya Mohammed Abdel Rahman amesema Baraza Kuu la Mahkama la serikali ambalo lina madaraka ya kutenguwa hukumu hiyo au hata kuwapa msamaha washtakiwa wataitafakari kesi hiyo hapo Jumatatu.

___________________________________________________________

Hakimu Fathi Dhan ameiambia kesi hiyo iliosikilizwa kwa dakika tano kwamba mahkama kuu hiyo imekataa rufaa ya washtakiwa na kuthibitisha adhabu hiyo ya kifo.Washtakiwa hao sita daktari mmoja wa Kipalestina na waaguzi watano wa Bulgaria walikuwa hawako mahkamani wakati hukumu hiyo ikitolewa.

Washtakiwa hao walihukumiwa adhabu ya kifo hapo mwezi wa Desemba baada ya kupatikana na hatia ya kuwaambukiza watoto wa Libya 426 virusi thakili vya HIV wakati walipokuwa wakifanya kazi kwenye hospitali ya watoto katika mji wa Benghazi katika miaka ya 1990.

Wakiwa wanasota gerezani tokea mwaka 1999 wanasema hawana hatia na kwamba waliteswa katika kuwalazimisha wakiri. Baadhi ya wanasayansi wa mataifa ya magharibi wanasema uzembe na hali ya uchafu kwenye hospitali hiyo ndio sababu za kutokea kwa janga hilo na kwamba waaguzi hao ni kisingizio tu.

Viongozi wa Umoja wa Ulaya na wale wa Bulgaria wameisikitikia hukumu hiyo ya leo katika mzonge wa karibuni kabisa katika kesi iliogeuzwa sana kuwa ya kisiasa lakini wanasema ufumbuzi bado unaweza kupatikana.

Matumaini yalikuwa makubwa ya kufanikisha makubaliano ya kuachiliwa kwao baada ya Wakfu wa Hisani wa Gaddafi uliposema hapo jana kwamba umefikia makubaliano na familia za watoto waathirika ambayo yameumaliza mzozo huo.

Maafisa wa Libya wanasema Baraza Kuu la Mahkama litakubali tu kuachiliwa kwa waaguzi hao iwapo kutafikiwa suluhisho katika mazungumzo ya faragha kati ya familia na Umoja wa Ulaya kwa ajili ya kugharamia matunzo ya afya kwa watoto hao ambayo Libya inayaita kuwa fidia wakati Bulgaria ikilikataa neno hilo kwa kuona kuwa limaanisha kwamba waaguzi hao wana hatia.

Kushindwa kuwaachiliwa kwa waaguzi hao kutamgharimu kidiplomasia kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi ambaye kwa miongo kadhaa alikuwa ametengwa na jumuiya ya kimataifa.

Familia za watoto waathirika wa Libya zimekuwa zikitaka zilipwe euro milioni 10 kwa kila mtoto kima kikubwa mno kuliko kile ilichokuwa tayari kulipwa na Umoja wa Ulaya.