1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maiti 40 zagunduliwa katika mji wa Bangui

27 Desemba 2013

Shirika la msalaba mwekundu limesema limegunduwa maiti zipatazo 40 katika mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika kati Bangui.

https://p.dw.com/p/1AhOs
Walinda amani 6,000 kutoka Afrika na Ufaransa wapelekwa Bangui.
Walinda amani 6,000 kutoka Afrika na Ufaransa wapelekwa Bangui.Picha: MIGUEL MEDINA/AFP/Getty Images

Kufuatia hali hiyo, Marekani imesema inawasiwasi wa kuzuka kwa mapigano mapya katika taifa hilo la kiafrika.

Kugunduliwa kwa maito hizo, kunakuja baada ya mapigano wakati zaidi ya watu elfu moja wakiwa wameuwawa katika mapigano ya wiki tatu baina ya Wakristo na waislamu.

Taarifa kutoka Shirika la habari la AFP zinasema kuwa miongoni mwa waliouawa, ni walinzi watano wa amani kutoka Chad,ambao walishambuliwa na wanamgambo wa Kikristo, wajulikanao kama 'anti-balaka' katika mji mkuu, Bangui, siku ya Jumatano.

Kufuatia kuzuka kwa mapigano hayo juzi, kulizusha hali ya wasi wasi miongoni mwa maelfu ya wakaazi wa mji wa Bangui ambao walilzamika kukimbilia katika eneo la Uwanja wa Ndege kwa ajili ya kupata hifadhi na vyakula, eneo ambalo walinda amani kutoka Ufaransa na Afrika wamepiga kambi.

John Kerry ataka kuitishwa uchaguzi haraka

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry, ameelezea wasiwasi wake juu ya mapigano hayo na kutoa wito kuitishwa kwa uchaguzi mara moja na kwamba kusuluhisha kwa njia ya mazungumzo inakuwa vigumu, huku watu wakiendelea kuangamia.

Uchaguzi ni suluhisho la haraka kumaliza mzozo-John Kerry.
Uchaguzi ni suluhisho la haraka kumaliza mzozo-John Kerry.Picha: picture-alliance/dpa

Akizungumzia kuawa kwa walinda amani kutoka Chad, msemaji wa kundi la Kimataifa linaloshughulikia mizozo, Thierry Vircoulon amesema, baadhi ya wapiganajii kutoka kundi la waasi la Seleka wameonekana wakiwa na vifaa vya mapigano wakitokea upande wa walipo walinda amani kutoka Chad ndipo yalipozuka mapigano kati ya waasi hao na walinda amani kutoka Chad.

Amesema mapigano ni makali ambapo pia baadhi ya waandamanaji wameuwa katika mji wa Bangui na ndiyo maana wameamua askari kutoka Chad kuondoka katika eneo hilo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na msemaji wa Shrika la msalaba mwekundu, David Pierre Marquet mbali ya mauaji hayo,takriban watu 30 pia wamejeruhiwa vibaya, na kwamba idadi hiyo ya vifo inaweza kuongezeka kutokana na kuendelea kwa mapigano.

Watu 1,000 wameripotiwa kuuawa

Kutokana na taarifa za Shirika la haki za binaadamu la Amnesty International kiasi cha watu 1,000 waliuawa katika siku mbili za ghasia mwanzoni mwa mwezi huu, ambapo Umoja wa Afrika na Ufaransa wamekwishapeleka wanajeshi 6,000 kurejesha amani.

Watu 700,000 walazimika kuyakimbia makaazi yao.
Watu 700,000 walazimika kuyakimbia makaazi yao.Picha: MIGUEL MEDINA/AFP/Getty Images

Wanamgambo kutoka makundi ya Wakristo na Waislamu wamekuwa wakipambana tangu kuangushwa kwa Rais Francois Bozize mwezi Machi mwaka huu, ambapo Rais wa kwanza Muislamu kwenye taifa hilo, Michel Djotodia, alichukuwa nafasi ya Bozize.

Takriban watu 700,000 katika Jamhuri hiyo ya Afrika ya Kati wamelazimika kuyakimbia mkaazi yao, ambapo idadi ya wakimbizi inazidi kuongezeka kwa mjibu wa Adrian Edwards kutoka Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa-UNHCR.

Mwandishi: Flora Nzema/AFP

Mhariri: Mohamed Abdul-Rahman