1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Mwisho mbaya ni mwanzo mbaya

Bruce Amani
22 Januari 2018

Mkutano mkuu wa SPD uliidhinisha mazungumzo rasmi ya kuunda serikali ya muungano. Lakini chama hicho kinasalia kugawanyika, na mbaya zaidi, uongozi wake unaonekana sasa kuwa dhaifu baada ya kura ya Bonn.

https://p.dw.com/p/2rH3j
Außerordentlicher SPD-Parteitag SPD-Fraktionsvorsitzende im Bundestag Andrea Nahles und SPD-Parteivorsitzender Martin Schulz
Picha: Reuters/W. Rattay

Martin Schulz, mwenyekiti wa chama cha Social Democratic, SPD anaashiria hali ya sasa ya chama chake;  hotuba yake ya saa nzima katika mkutano mkuu wa SPD mjini Bonn ilikosa matumaini na msisimko, miongoni mwa wajumbe 600 walioshiriki. Schulz, ambaye mwaka mmoja uliopita aliacha jukumu lake kuwa rais wa bunge la Ulaya ili kuwa kiongozi wa SPD na kukiweka chama hicho katika hali ya kusifiwa, sasa amesimama kwa kuegemea mgongo wake kwenye ukuta. Amepata pigo la kisiasa. Anaonekana mwenye uchovu mwingi.

Tawi la vijana wa SPD, wanapinga vikali chama hicho kuungana tena na wahafidhina wa Merkel katika serikali ya muungano. Upinzani wao usiofaa kama walivyohoji baadhi ya viongozi wa chama, bila shaka uliungwa mkono na idadi kubwa ya wajumbe. Asilimia 44 yao walipiga kura kupinga kuanzishwa mazungumzo rasmi ya muungano. Ni asilimia 56 pekee waliokubali pamoja na kiongozi wa chama na watendaji wengine waliounga mkono mazunguzmo ya muungano.

Andrea Nahles: Chaguo bora la kuwa kiongozi wa chama?

Außerordentlicher SPD-Parteitag SPD-Fraktionsvorsitzende im Bundestag Andrea Nahles
Andrea Nahles akiwahutubia wajumbe wa SPD BonnPicha: Reuters/W. Rattay

Hili haliendani vyema na chama hicho na uongozi wake. Tayari, mpasuko mkubwa umekigawa chama cha SPD. Na mpasuko huu utakuwa kubwa kadri muda unavyosonga. Ndani ya chama, kambi mbili zenye fikira tofauti zinagombana. Pande zote zina hoja nzuri. Lakini misimamo yote inakuja na hatari zake. Kuunda upya muungano na chama cha Kansela Angela Merkel cha Christian Democratic Union – CDU na chama ndugu kutoka Bavaria cha Christian Social Union, CSU kunaweza kukidhoofisha SPD. Vile vile uchaguzi mpya huenda ukawadhoofisha wana SPD. Hakuna suluhisho bora. Ni kizungumkuti.

Itasubiriwa kuona kama Martin Schulz ataweza kuikwamua SPD kutoka kwenye mgogoro huu mkubwa kabisa katika historia ya chama hicho. Andrea Nahles, ambaye anaongoza SPD katika bunge la Ujerumani, huenda akaweza kuitatua changamoto hiyo. hotuba yake yenye shauku na nzito katika mkutano wa Bonn ilikuwa kitu alichoshindwa kufanya Schulz. Ujumbe wake na mkazo wa hotuba vilipongezwa na wajumbe. Huenda hata aliweza kuwashawishi baadhi ya waliokuwa na mashaka wakati aliahidi kuwa mazungumzo ya muungano yatakuwa mapambano hadi mwisho.

Kinkartz Sabine Kommentarbild App
Mwandishi wa DW Kinkartz Sabine

Kulikuwa na wengi wenye mashaka miongoni mwa wajumbe wa mkutano huo wa Bonn. Wale ambao waziwazi wanapinga muungano ni wagumu kuwashawishi vinginevyo. Lakini kwa kiasi kikubwa sio wote waliounga mkono kwa dhati muungano mpya. Bado kuna mashaka. Waliopiga kura ya kuanzishwa mazungumzo ya muungano, na hivyo serikali ya muungano walifanya hivyo kwa sababu ilikuwa bora ukilinganisha na hali iliyopo.

Na wanachama 450,000 watakaoyapigia kura makubaliano ya mwisho ya muungano, pia, watakabiliwa na hali ngumu katika kuchagua kipi bora Zaidi. Lakini ni vipi chama kilichogawika kiasi hicho kinaweza kuongoza nchi? Chama ambacho wanachama wa kawaida wanawavuruga uongozi wake? Wana SPD ambao wameendelea kudhoofika katika miaka ya karibuni, lazima wawe makini. Kwa sasa hawana furaha. Lakini kama chama hicho kitashindwa kurejea kwenye mkondo wa kujifufua, wapiga kura huenda wakakosa Imani yao yote katika SPD na kukitokomeza kabisa chama hicho

Mwandishi: Sabine Kinktartz

Tafsiri: Bruce Amani/DW http://bit.ly/2rwnROG
Mhariri: Grace Patricia Kabogo