1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wawakilishi wa serikali ya Afghanistan hawajaruhusiwa

1 Mei 2019

Mazungumzo mapya yanaendelea baina ya Marekani na Taliban mjini Doha nchini Qatar kwa lengo la kusitisha vita vilivyodumu kwa muda mrefu vya Marekani nchini Afghanistan.

https://p.dw.com/p/3Hm8N
Russland Friedensgespräche Afghanistan | Taliban-Delegation in Moskau
Picha: Reuters/S. Karpukhin

Mazungumzo hayo yanajiri wakati shinikizo zinaendelea za kutafutwa kwa mpango wa kusitisha vita hivyo vilivyodumu kwa muda wa miaka kumi na saba sasa na bado vinaendelea kuwa vibaya.

Msemaji wa kundi la Taliban, Zabiullah Mujahid, alisema katika kikao hicho ni wawakilishi wa Marekani na Taliban na baadhi ya maafisa wa Qatar ambao ndio wenyeji wao, ila wawakilishi wa serikali ya Afghanistan hawajaruhusiwa kwa sababu Taliban wanaichukulia serikali ya Afghanistan kama kikaragosi cha Marekani.

Katika kikao hicho kinachoendelea, mjumbe maalum wa Marekani wa amani nchini Afghanistan, Zalmay Khalilzad, na wajumbe wake wanajikita zaidi katika azimio la kusimamisha mapigano kama njia ya kwanza ya kumaliza vita hivyo.

USA Zalmay Khalilzad in Washington
Mjumbe maalum wa Marekani wa amani nchini Afghanistan, Zalmay Khalilzad,Picha: picture-alliance/AP Photo/J. Martin

Afisa anayefanya kazi kwa ukaribu na Khalilzad alisema mjumbe huyo anatarajiwa kulihimiza kundi hilo la waasi kuanza mazungumzo na viongozi wa kisiasa nchini Afghanistan ili kupata muafaka wa kisiasa wa kukomesha vita hivyo.

Rais Ashraf awaita Taliban kwa mazungumzo

Sambamba na mkutano huo nchini Afghanistan, Rais Ashraf Ghani wiki hii aliandaa kongamano mashuhuri la Loya Jirga, linalowajumuisha wanasiasa, viongozi 3, 200 wa makabila mbali mbali, viongozi wa kijamii na wakidini kutoka mikoa yote 34 kujadili masharti ya vikao vya amani na Taliban. Rais Ashraf amewapa changamoto Taliban kujitokeza kufanya naye mazungumzo.

"Matarajio ya watu ni kuyajadili haya maswala ya amani na ustawi kwa njia ya kidungu baina yenu. Natoa changamoto kwa Taliban kwamba wao ni waisilamu na kuwa ni raia wa Afghanistan kwamba hakuna swala la watu wanje ya Afghanistan, kwa nini munaogopa kujadiliana na taifa la Afghanistan na serikali?", alisema rais Ashraf.

Mazungumzo hayo ni kati ya juhudi za rais Donald Trump katika kusitisha vita hivyo vilivyoanza mwaka 2001 wakati jeshi la Marekani liliwaondoa madarakani Taliban wiki kadhaa baada ya shambulizi la Septemba 11.

Tangu mwezi Oktoba mwaka jana, Marekani na Taliban wamekuwa na mazungumzo ya kuweka njia salama kwa vikosi vya marekani kutoka ila kwa sharti la Taliban kuihakikishia Marekani kwamba Afghanistan haitatumiwa na makundi yaliyo na silaha kutishia ulimwengu.

(RTRE/AFPE)