1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani,Taliban wasaini makubaliano ya amani mjini Doha

Daniel Gakuba
29 Februari 2020

Baada ya mazungumzo ya zaidi ya mwaka mzima, Marekani imesaini makubaliano na kundi la Taliban, yanayosafisha njia kwa Marekani kuondoa wanajeshi wake nchini Afghanistan. Makubaliano hayo yamesainiwa mjini Doha, Qatar.

https://p.dw.com/p/3Yemd
Katar Unterzeichnung Abkommen USA mit Taliban
Picha: AFP/G. Cacace

Marekani na kundi la wanamgambo wa Taliban leo wametia saini makubaliano ya amani yanayolenga kumaliza vita vya miaka 18 nchini Afghansitan na kuwezesha Marekani kuondoa wanajeshi wake nchini humo.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo pamoja na msemaji wa kundi la Taliban mjini Doha, Suhail Shaheen walikuwepo wakati makubaliano hayo yaliposainiwa.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mike Pompeo ametoa wito kwa Taliban kuheshimu ahadi ilizotoa ikiwa ni pamoja na kukomesha mahusiano yake na makundi ya itikadi kali.

Chini ya mkataba huo Marekani itaanza kuondoa wanajeshi wake kwa makubaliano ya Taliban kuzuia mashambulizi ya kigaidi dhidi ya Afghanistan.

Pindi kundi la Taliban litatimiza masharti ya mkataba huo Marekani itaondoa wanajeshi wake wote ndani ya muda wa miezi 14 inayokuja.

Wadau wasifu hatua iliyopigwa

Pande zote mbili, Marekani na Wataliban, zimesifu hatua hiyo iliyopigwa zikiitaja kuwa ya kihistoria, na ambayo itasaidia kurejesha amani baada ya miaka mingi ya vita nchini Afghanistan.

Siku moja kabla ya kusainiwa makubaliano hayo, rais wa Marekani Donald Trump alisema ''ikiwa Wataliban na serikali ya Afghanistan wataendelea kuheshimu makubaliano haya, hali hiyo itaipeleka Afghanistan katika njia thabiti ya amani, itakayowesha Marekani kurejesha nyumbani wanajeshi wake'.

Kutiwa saini mkataba huo kunatimiza moja ya ahadi muhimu ya wakati wa uchaguzi iliyotolewa na rais Donald Trump ya kuindoa Marekani kutoka vita visivyokwisha ikiwemo nchini Afghanistan, na wachambuzi wanaiona kama turufu ya rais huyo kuelekea uchaguzi mkuu ujao atakapokuwa akiwania muhula wa pili madarakani.

Umoja wa Ulaya umesema unaunga mkono hatua ya kufikiwa makubaliano hayo baina ya Marekani na Watalibani, lakini ikahimiza kuendelea kuheshimiwa kwa haki za binadamu na za wanawake nchini Afghanistan.