1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashabiki uwanjani Wembley na virusi vya corona

Tatu Karema
5 Julai 2021

Mechi tatu za mwisho za michuano ya kombe la Euro 2020 zitachezwa mbele ya mashabiki elfu 60 katika uwanja wa Wembley lakini sababu mbalimbali zinadidimiza furaha ya kuitazama michuano hiyo .

https://p.dw.com/p/3w3rH
EURO 2020 | Ukraine vs England | englische Fans in Rom
Picha: Marco Iacobucci/PA Images/imago images

Uwezekano wa mashambiki elfu 60 kuwepo katika uwanja wa Wembley kutazama nusu fainali za michuano hiyo ya Euro 2020 pamoja na fainali baadaye wiki hii, umeibua wasiwasi kwa baadhi ya watu huku wengine wakitaka sana kuwa miongoni mwa mashabiki watakao hudhuria mechi hizo. Ongezeko la mashabiki kutoka zaidi ya elfu 20 wakati wa mechi za makundi hadi kufikia mashabiki elfu 45 katika mechi za muondoano kunatokea wakati ambapo visa vya maambukizo vinazidi kuongezeka huku serikali ya Uingereza ikisema Jumatatu kuwa inapanga kuondoa sheria nyingi za udhibiti wa virusi hivyo mnamo Julai 19.

Lakini huku udhibiti wa usafiri ukiwa bado umedumishwa kufikia sasa, inamaanisha kuwa mechi ya nusu fainali kati ya Uhispania na Italia siku ya Jumanne na Uingereza dhidi ya Denmark zitaweza kuhudhuriwa na mashambiki wanaoishi Uingereza pekee kwa kuwa watu kutoka nchi nyingine wanapaswa kuwa chini ya karantini kwa siku tano. Watu wa pekee watakaoruhusiwa ni kutoka visiwa wa Balearic vya Uhispania wanaoruhusiwa kuingia Uingereza kwa kuonesha tu cheti kinachothibitisha kutokuwa na maambukizo ya virusi vya corona.

Denmark yaendeleza juhudi za kusafirisha mashambiki

Hali hiyo inaipa Uingereza faida kubwa ya uwanja wa nyumbani lakini Denmark bado haijafutilia mbali juhudi za kuwasafirisha mashabiki wake kwa mechi hiyo ya Jumatano. Waziri mkuu Mette Frederiksen na waziri wa mambo ya nje Jeppe Kofod wamehimizwa kuzungumzia kuhusu mashambiki hao huku gazeti la nchi hiyo la Ekstra Bladed likiripoti Jumatatu kwamba watu wamepata chamjo, kupimwa na tayari kusafiri. Tiketi elfu 5 zimepangiwa mashambiki wa Denmark walioko Uingereza na mipangilio kama hiyo ikifanyiwa mashabiki wa Italia na Uhispania. Kutakuwa na sheria tofauti kidogo kwa mechi ya fainali ya siku ya Jumapili.

EURO 2020 | Ukraine vs England | Fans in London
Mashabiki wa mechi kati ya Ukraine na Uingereza mjini LondonPicha: REUTERS

Serikali ya Denmak imesema kuwa huenda mashabiki elfu moja wakasafiri kwa ndege na kuhudhuria mechi hiyo huku wakiwasili na kuondoka siku hiyo ya mechi. Kumekuwa na shtuma kali kuhusu idadi ya mashambiki na usafiri wote wakati wa michuano hiyo katika miji 11 ya bara Ulaya huku mashambiki kutoka mataifa mbali mbali wakirejea nyumbani wakiwa na maambukizo ya virusi vya corona. Viwango vya maambukizo vinaongezeka tena nchini Uingereza huku asilimia 90 ikiwa ni ya virusi vya delta na visa elfu 24 vya maambukizo vikiripotiwa siku ya Jumapili.

Serikali ya Uingereza yanuia kulegeza sheria za kudhibiti corona

Hata hivyo serikali ya waziri mkuu Boris Johnson inanuia kulegeza sheria za kudhibiti maambukizo na kuruhusu watu kuingia katika ukumbi wa sinema, vilabu na maeneo ya michezo bila ya barakoa na hatua ya kuweka umbali wa mtu mmoja hadi mwingine. Profesa Christina Pagel kutoka chuo kikuu cha London, ambaye ni mmoja wa wanachama wa jopo la ushauri la serikali. amepuuzilia mbali haya na kusema ni mpango mbaya kwasababu utategemea mpango wa chanjo pekee ambapo asilimia ni 64 ya idadi ya watu walio na umri wa zaidi ya miaka 18 waliopata chanjo zote mbili huku asilimia 87 ikipata chanjo moja.

Shirikisho la kandanda la Ulaya UEFA lilisisitiza kabla ya michuano hiyo kwamba mashambiki waruhusiwe kuhudhuria hali iliyopelekea jamhuri ya Ireland na Uhispania kupoteza hadhi yao ya kuandaa michuano hiyo lakini sasa shirikisho hilo linategemea maamuzi ya serikali husika. Waziri wa mambo ya ndani wa Ujerumani Horst Seehofer ametaja msimamo huo kuwa wakutowajibika huku mkurugenzi wa shirika la afya duniani WHO barani Ulaya Hans Kluge akisema kuwa wana wasiwasi kuhusu michuano hiyo.

Lakini michuano hiyo ya Euro ni sehemu ya majaribio kadhaa ya michuano mikubwa nchini Uingereza kuhusu kurudi kwa mashambiki kama vile Wimbledon ambapo ukumbi wa kati na wa kwanza inaweza kujaa mashabiki kutoka robo fainali siku ya Alhamisi na kuendelea.