1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashindano ya riadha Osaka

Ramadhan Ali27 Agosti 2007

Kenenisa Bekele atamba tena katika mita 10.000 wakati taji la mwanamke wa kasi duniani laenda kwa Veronica Campbell wa Jamaica.

https://p.dw.com/p/CHb9
Kenenisa Bekele
Kenenisa BekelePicha: AP Photo/Mark Baker

Kenya ilikua ya kwanza kutoroka na medali ya dhahabu pale Luke Kibet alipotamba katika mbio za marathon .

Katika mbio za mita 100,Gary Tyson wa Marekani, amemtimua nje bingwa wa rekodi ya dunia Asafa Powel wa Jamaica.Bayern Munich waikomea Hannover 96 3:0 na kubakia kileleni.

MASHINDANO YA RIADHA YA DUNIA:

Medali 5 za dhahabu zimeaniwa hii leo lakini msisimko ulituwama katika mbio za mita 10.000 ambamo muda mfupi uliopita muethiopia Kenenisa Bekele kama ilivyotarajiwa, alinyakua ushindi wake 3 mfululizo wa mbio za mita 10.000.

Bekele alichomoka mbio zikisalia mita 200 ili kumpita Sileshi Sihine pia wa Ethiopia alieonekana kana kwamba ushindi ni wake.Muda wake ulikua dakika 27.05.90.Mkenya Irungu Mathathi alimaliza 3 na kutwaa medali ya shaba kwa Kenya.

Kenenisa Bekele tayari ni bingwa wa rekodi wa dunia wa mita 5000. Kenenisa sasa anaziandama medali 4 za dhahabu alizozinyakua mtangulizi wake Gebreselassie kati ya 1993 hadi 1999.

Hapo kabla jumamosi,muethiopia mwengine-msichana Tirunesh Dibaba alinyakua medali ya kwanza ya dhahabu kwa Ethiopia katika mashindano haya ya Osaka,alipotokla nyuma na maumivu ya tumbo na mwishoe kuwa mwanamke wa kwanza kutetea taji lake la mita 10.000 la ubingwa wa dunia.

Dibaba alikuwa pia mwanamke wa kwanza kushinda masafa yote 2 –mita 5000 na 10.000 miaka 2 nyuma huko Helsinki.

Dibaba alimpita muethiopia anaekimbia chini ya bendera ya Uturuki, Elvan Abyelegesse aliebidi kuridhika na medali ya fedha.Ushindi wa dibaba unaseleleza rekodi ya Ethiopia kushinda masafa haya tangu 1999.dada yake mkuu Ejegayehu Dibaba ,alieshinda medali ya fedha ya olimpik 20004 huko Athens,mara hii alimaliza nafasi ya 7 na bila medali.

Ushindi wa Tirunesh Dibaba hapo jumamosi, ulifunguliwa mlango na mkenya Luke Kibet katika mbio za marathon.Kibet alifuatwa na mzaliwa wa Kenya aliekimbia kwa niaba ya Qatar Mubarak hassan Shami. Kenya imenyakua leo medali ya pili ya shaba katika mbio za mita 3000 kuruka viunzi.Eunice Jepkorir alikuja nyuma ya mshindi Yekaterena Volkova na Tatyana Petrova wote kutoka Russia.

Changamoto ya mita 100 kuamua nani ni mwanadamu wa kasi kabisa kati ya bingwa wa rekodi ya dunia Asafa Powell wa Jamaica na chipukizi wa Marekani Tyson Gay,ilimalizika kwa ushindi wa Gay kwa muda wake wa sek.9.85.

Derrick Atkins alimpiku pia Powell na kunyakua medali ya fedha huku Powell akibidi kuridhika na medali ya shaba.Muda wake ulikua sek.9.96.Si Powell wala Gay waliowahi kutwaa taji la dunia hapo kabla.Changamoto nyengine kati yao yatazamiwa kuwa mjini Brussels,Ubelgiji mwezi ujao.

X:Ushindi wa Veronica Campbell,uliamuliwa kwa picha-foto-finish,kwani ilikua vigumu kuamua nani amempiku mwenzake mfundoni. Lauryn Williams wa Marekani alikuja wapili ingawa muda sawa na Compbell. na Kamelita Jeter akaja 3.

Katika Bundesliga-Ligi ya Ujerumani,Bayern Munich, yabainika imeanza msimu kwa kishindo baada ya kuirarua Hannover 96 hapo jumamosi kwa mabao 3:0 uwanjani Allianz Arena.

Munich iliufumania kwanza mlango wa Hannover mnamo dakika ya 28 ya mchezo pale mtaliana Luca Toni alipopiga hodi na kuitiwa.

Mabingwa Stuttgart waliondoka na ushindi wao wa kwanza msimu huu pale mshambulizi wao Mario Gomez alipokomea bao pekee katika lango la Duisburg.Schalke 04,makamo-bingwa,hawakuwa na bahati walipoondoka suluhu bao 1:1 na Wolfsburg. Alikuwa mturuki Halil Altintop aliewaokoa dakika 4 kabla ya firimbi ya mwisho kulia.

Katika premier League-Ligi ya Uingereza,mabingwa Manchester United waliondoka na ushindi wao wa kwanza msimu huu walipoitimua jana Tottenham Hotspur kwa bao 1:0.

Firimbi imelia kwa changamoto za kombe lijalo la dunia nchini afrika Kusini kanda ya Afrika:

Madagascar itaumana na jirani zao Comoro wakati Seyschelles ina miadi na Jibouti.Somalia itacheza na Swaziland wakati Sierra leone itaumana na Guinea Bissau katika duru za kwanza kabisa.Jamhuri ya Afrika ya kati ina miadi na sao Tome .