1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wito wa kutunza msitu wa Amazon watolewa Brazil

Bruce Amani
9 Agosti 2023

Mataifa nane ya eneo la msitu wa Amazon yametoa wito kwa nchi zilizostawi kiviwanda kuongeza juhudi za kusaidia kuutunza msitu huo mkubwa kabisa ulimwenguni.

https://p.dw.com/p/4Uwln
Brasilien | Protest gegen die Ölexploration in der Region
Picha: Nádia Pontes

Yametoa kauli hiyo katika mkutano wa kilele nchini Brazil wa kujadili juhudi za pamoja za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

Viongozi wa mataifa ya Amerika Kusini ambayo yanautumia msitu wa Amazon, walihitimisha mkutano wao wa siku mbili mjini Belem, kwa kusema kuwa jukumu la kukomesha uharibifu wa msitu huo wa mvua haliwezi tu kuwa la nchi chache ilhali mzozo huo umesababishwa na wengi.

Nchi za msitu wa Amazon zakutana kujadili ulinzi wa eneo hilo

Miito ya wanachama hao wa Shirika la Mkataba wa Ushirikiano wa Amazon, ACTO imejiri wakati viongozi wakilenga kuchochea maendeleo ya kiuchumi yanayohitajika sana katika maeneo yao huku wakizuia uharibifu unaoendelea wa msitu wa Amazon kufikia hatua ya kutorudi nyuma.

Wakosoaji hata hivyo wamesema tamko hilo halijakwenda mbali ya kinachohitajika ili kuutunza msitu huo. Tamko hilo la pamoja liliunda muungano wa kukabiliana na ukataji miti, lakini likaiacha kila nchi kuyatekeleza malengo yake yenyewe ya uhifadhi wa mazingira.