1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matokeo kutoka viwanja vya dimba

22 Juni 2007

Timu kadhaa zajinoa kwa msimu mpya wa dimba huku wachezaji wakihamia klabu mpya .Timu kadhaa za taifa zimepanga miadi kukutana kirafiki.

https://p.dw.com/p/CHbu

Baada ya Al Ittihad ya Libya na JS Kabylie ya Algeria kufungua ijumaa duru ya mwishoni mwa wiki hii ya kinyan ‘ganyiro cha kombe la klabu bingwa barani Afrika katika kundi A, Esperence ya Tunisia na ASEC MIMOSAS ya Ivory Coast zinaumana leo huko Tunis.

Kesho itakua zamu ya kundi B kwa mabingwa wa Afrika Al Ahly ya Misri kupapurana na Al Hilal ya Sudan.

Finali ya Kombe la CONCACAF-shirikisho la dimba la kanda ya Amerika ya kati na kaskazini itakua kwa mara ya tatu kati ya Mexico na Marekani.Marekani iliipiga kumbo nje ya finali Kanada juzi alhamisi ili kuweka miadi na Mexico ilioitoa Guadelope kwa bao 1:0.Marekani ilizaba Kanada 2:0.

Simba wa nyika- Kamerun wana miadi nao ya kukutana na Japan August 22.Mpambano wao huo unafuatia kukata kwao tiketi ya kombe lijalo la Afrika la mataifa mwishoni mwa wiki iliopita walipoitimua Rwanda huko garua,Kamerun.Mpambano na japan utachezwa huko Kyushu.

Stadi wa Ivory Coast, Yaya Toure atajiunga na FC Barcelona msimu ujao.Meneja wa toure Dimitri Selluyk akitazamiwa kwenda Barcelona jana kukamilisha mkataba.Ikitazamiwa pia kwamba toure mwenye umri wa miaka 24 angewasili kesho huko Barcelona kwa ukaguzi wa afya yake.Taarifa zasema Barcelona itabidi kuilipa Monaco ya Ufaransa euro milioni 12 kumkomboa Toure.

Taarifa nyengine kutoka Barcelona,makamo-bingwa wa Spain, zasema rais wake Joan Laporta amehuzunishwa kuona mastadi wa 2 wqa FC Barcelona-mkamerun Samuel Eto’o na mbrazil Ronaldinho hawakuhudhuria mapokezi ya timu ya Barcelona na mzee Nelson Mandela wa afrika kusini.

Ni walinzi Lilian Thuram,Oleguer,Giovanni van Brockhorst,Juliano Beletti na mchezaji wa kiungo Andreas Iniesta walikwenda kumtembelea mzee Mandela mwenye umri wa miaka 88.

Msimu wa mpya ukijongelea,timu mbali mbali zimeanza kujinoa na kujiimarisha kwa kuwaajiri mastadi wapya na kuachana na baadhi yaw a zamani:

Mbrazil Ze Roberto,jana alifunga mkataba wa miaka 2 na klabu yake ya zamani Bayern Munich na hivyo, anarejea msimu ujao katika Bundesliga-Ligi ya ujerumani.Ze akiwa na umri wa miaka 32 alijiunga na Munich 2002 kutoka Bayer Leverkusen na alishinda mataji 3 ya Ligi na kombe 1 la shirikisho akiichezea Bayern munich.

Ze Roberto aliiachamkono Bayern Munich mwaka jana pale waliposhindwa kuafikiana masharti ya mkataba mpya.Munich imejiimarisha kwa msimu ujao baada ya msimu uliopita kuwaendea kombo na kumaliza 4.Imewaajiri kwa msimu ujao akina Franck Ribery wa timu ya taifa ya Ufaransa, Luca Toni, wa mabingwa wa dunia-Itali,mturuki Hamit Alintop na Muargentina Jose Sosa.

Mbrazil mwengine Lincoln,mchezaji wa kiungo anaiachamkono Schalke amefunga jana mkataba na Galatasary,Istanbul ya Uturuki kwa kitita cha Euro milioni 5.Lincoln alikuwa katika kikosi cha kwanza cha wachezaji 34 kilichochaguliwa na kocha wa Brazil, Dunga kwa Copa America-kombe la Amerika kusini.

Wakati Lincoln anahamia Uturuki,stadi mwengine wa Brazil, Juan anaejiandaa sasa kucheza katika Copa America anaiacha bayer Leverkusen kuhamia AS Roma ya Itali.Ikiwa sehemu ya biashara hiyo, Roma itaitembelea Leverkusen kwa mpambano wa kirafiki hapo Julai 29.

Werder Bremen inayozozana bado na Bayern Munich juu ya hatima ya mshambulizi wa timu ya taifa Miroslav klose,ina miadi na Everton ya Uingereza Julai 31 kwa mpambano wa kirafiki.Everton ilimaliza nafasi ya 6 katika Premier League-ligi ya Uingereza- wakati Bremen, ilimaliza nafasi ya 3 nyuma ya mabingwa Stuttgart na makamo-bingwa Schalke .