1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chuki dhidi ya Wayahudi yameongezeka Ujerumani

28 Novemba 2023

Jumla ya matukio 994 ya chuki dhidi ya Wayahudi yameripotiwa nchini Ujerumani katika mwezi wa kwanza wa vita kati ya Israel na kundi la wanamgambo la Hamas.

https://p.dw.com/p/4ZY2o
Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akiwa na rais wa Baraza la Wayahudi Ujerumani Josef Schuster.
Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akiwa na rais wa Baraza la Wayahudi Ujerumani Josef SchusterPicha: John Macdougall via REUTERS

Kwa mujibu wa muungano wa idara za utafiti inayokusanya matukio ya chuki dhidi ya Wayahudi RIAS, ni kwamba Ujerumani inaripoti matukio ya chuki 29 kwa siku, idadi hiyo ikiwa zaidi ya asilimia 320 ya wastani wa kila siku ya rekodi zilizokusanywa mwaka 2022.

Utafiti huo ulifanyika katika ya Oktoba 7 hadi Novemba tarehe 9 mwaka huu. RIAS imeeleza kuwa Wayahudi wengi walikabiliwa na matukio ya chuki na kwamba maisha yao yako hatarini.

Soma pia:Ulaya yakabiliwa na ongezeko la chuki dhidi ya Wayahudi

Mjini Giessen kwa mfano, wanaume wawili waliingia kwenye nyumba na kuiondoa bendera ya Israel iliyokuwa inaning'inia nje ya dirisha.

Matukio ya chuki dhidi ya Wayahudi na propaganda dhidi ya Israel pia yameongezeka katika vyuo vikuu. Wanafunzi Wayahudi wameeleza kuwa, wanafunzi wenzao wamewalaumu kwa vitendo vinavyofanywa na serikali ya Israel huku wanafunzi wengine wakiacha kabisa masomo.