1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matumaini ya amani ya mashariki ya kati

Oumilkher Hamidou2 Septemba 2010

Vizingiti viwili vikubwa -ujenzi wa makaazi ya wayahudi na makundi ya itikadi kali-vinaweza kuutia munda utaratibu wa amani-wanahofia wadadisi

https://p.dw.com/p/P2q8
Kiongozi wa utawala wa ndani wa Palastina Mahmud Abbas na waziri mkuu wa Israel Benjamin NetanyahuPicha: ap

Waisrael na Wapalastina wamerejea katika meza ya mazungumzo na hadi wakati huu maoni yanayotolewa yanaonyesha kutia moyo.

Waziri mkuu Benjamin Netanyahu anazungumzia juu ya amani ambayo kila mmoja atafaidika na anasema "amani inaweza kupatikana."

Rais Mahmoud Abbas anasema wapalastina wanataka kumaliza mgogoro wa Mashariki ya kati.

Rais Barack Obama,mwenyeji wa mazungumzo hayo,amezitolea mwito pande zote mbili zisiitupe fursa ya kufikia amani.

Lakini kishindo kama mazungumzo yatafanikiwa,kama mazungumzo ya siku mbili ya amani mjini Washington yatapelekea kupatikana amani ya kweli-si jambo linalotegemea maoni ya umma.

Pekee kama wajumbe mazungumzoni watajifungia ndani ya chumba na kujadiliana ndipo watu wanavyoweza kukadiria nafasi ya kweli ya kupatikana amani katika duru hii ya mazungumzo kati ya Israel na Palastina.

Mazingira ya kabla ya mazungumzo ya Washington hayakuwa ya kutia moyo.Wachache tuu ndio waliokua wakificha hofu walizo nazo na hakuna upande wowote uliokua ukificha hisia zake kuelekea upande wa pili.

Lakini hata kama mazungumzo ya jana yamepita vizuri na kila mmoja ameonekana anatabasamu na kuzungumzia jinsi walivyopania kuufumbua mgogoro huo,bado watalazimika kukabiliana na mada mbili zinazogubika utaratibu wa amani na ambazo pengine zikawa sababu ya kumalizika kwa ghadhabu utaratibu huo.

Kitisho cha kwanza na ambacho pengine ni kikubwa kupita kiasi ni kuhusu kusitishwa ujenzi wa makaazi ya wahamiaji wa kiyahudi katika maeneo ya ukingo wa magharibi-muda uliowekwa na waziri mkuu Benjamin Netanyahu utakapomalizika September 26 ijayo.

Wapalastina wametishia kujitoa mazungumzoni ikiwa muda huo hautarefushwa.Baadhi ya washirika katika serikal ya Benjamin Netanyahu wametishia kujitoa katika serikali ya muungano ikiwa muda huo utarefushwa.

Kwa hivyo kila upande unaweza kukitumia kisa hicho cha ujenzi wa makaazi ya wayahudi ili kupima subira ya upande wa pili.

September 26 ndio itakayotupatia jibu kwa jinsi gani suala hilo ni tete.

Nahost / Palästinenser / Israel / Gazastreifen / Westjordanland
Wafuasi wa kundi la itikadi kali la HamasPicha: AP

Kitisho chengine kinahusu makundi ya wanamgambo wanaoungwa mkono na Iran-makundi ambayo kama ilivyokua miaka ya nyuma,wanachama wake wamedhamiria kuufuja utaratibu wa amani ambao hawauungi mkono.

Mashambulio mawili yamefanywa katika Ukingo wa magharibi-ambapo waisrael wanne wameuliwa na wawili kujeruhiwa-Hamas wamesema walikua nyuma ya mashambulio hayo.

Mashambulio hayo-na Hamas wanasema wataendelea kuhujumu,yanabainisha ukweli kwamba ikiwa makundi ya wanamgambo yanayopinga maridhiano pamoja na Israel,hayatavunjwa nguvu,amani,hata kama ikipatikana, itakuwa shida au hata muhali kuitekeleza.

Mwandishi: Hamidou Oummilkheir /dpa

Mpitiaji:Mohammed Abdul-Rahman