1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matumaini ya Wazanzibari katika urais wa Samia Suluhu Hassan

Salma Said19 Machi 2021

Licha ya huzuni iliyotanda Tanzania na Zanzibar, kufuatia kifo cha Rais John Magufuli, Wazanzibari wamepata matumaini makubwa baada ya kuapishwa kwa Mzanzibari mwenzao Samia Suluhu Hassan kuwa rais wa muungano.

https://p.dw.com/p/3qsmx
Tansania Daressalam | Amtseinführung neue Präsidentin Samia Suluhu Hassan
Picha: STR/AFP/Getty Images

Ni kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania kwa mwanamke kushika wadhifa huo wa urais. 

Baada ya kuapishwa kwa Mama Samia saa nne asubuhi, watu mbali mbali walifuatilia matangazo ya moja kwa moja yaliokuwa yakirushwa na vituo vya televisheni na kuonesha kufurahishwa kwao.

Baadhi ya watu walikuwa wakitoa kauli za kumshukuru Mungu kwa hatua hiyo iliyofikiwa huku wengi wakitoa maoni yao kuonesha matumaini makubwa na kumtakia kheri kwenye utumishi wake.

Watu ambao amefanya nao kazi wanamzungumzia Rais Samia kuwa ni mchapakazi, msikivu, mwenye tabia ya kuheshimu maamuzi yanayotokana na vikao na mtoaji maamuzi yasioumiza kutokana na kutumia busara zaidi kwenye uamuzi wake. Professa Mohammed Hafidh Khalfan ambayee ni mmoja wa waliofanya naye kazi, amesifia utendaji wake wa kazi.

Samia Suluhu Hassan akila kiapo cha urais katika ikulu ya Dar es Salaam 19.03.2021
Samia Suluhu Hassan akila kiapo cha urais katika ikulu ya Dar es Salaam 19.03.2021Picha: Stringer/REUTERS

Baadhi ya wanaharakati akiwemo Jamila Mahmoud ambaye ni mkurugenzi wa wanasheria wanawake (ZAFELA) wamefurahishwa na wanaona nafasi hiyo inaweza kubadilisha na kuleta mtazamo mpya wa kuondokana na mfumo dume.

Samia alikuwa mwanamke wa kwanza kuwa makamu wa Rais na sasa ameongeza rekodi ya kuwa Rais wa kwanza Tanzania mwanamke.