1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya amani ya mashariki ya kati yaendelea

Sekione Kitojo15 Septemba 2010

Mazungumzo ya ana kwa ana kati ya waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na rais Mahmoud Abbas wa Palestina leo yameingia katika siku yake ya pili mjini Jerusalem.

https://p.dw.com/p/PCvu
Rais wa Israel Shimon Peres, akizungumza na waandishi habari akiwa pamoja na waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Hillary Rodham Clinton, mjini Jerusalem.Picha: AP

Mazungumzo  ya ana kwa ana  kati ya Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na Rais Mahamoud Abbas wa Palestiana leo yameingia katika siku ya  pili, mjini Jerusalem. Mazungumzo hayo ambayo ni duru ya pili yalianza jana huko Sharm el-Sheikh-Misri. Lakini ujenzi  wa vitongoji  vya  makaazi  ya  Wayahudi , ambao  unatishia kuivunja  duru  ya  hivi  sasa  ya  mazungumzo  ya kutafuta  amani  ya  mashariki  ya  kati  yanayosimamiwa na  Marekani , umewakasirisha  Wapalestina  pamoja  na mataifa  mengi  ya  Kiarabu   tangu  pale  ujenzi  huo ulipoanza  miaka  40  iliyopita.

Wapalestina  wanaona  kuwepo  kwa   Waisrael  nusu milioni   katika  vitongoji  zaidi  ya  120  vilivyotawanyika katika   maeneo  yanayokaliwa  kimabavu  na  Israel pamoja  na  eneo  lililotekwa  la  Jerusalem  ya  mashariki ni  tishio  kubwa  dhidi  ya  kuundwa  kwa  taifa  la  baadae la  Wapalestina.

Jumuiya   ya  kimataifa , ikiwa  ni  pamoja  na  mshirika  wa karibu  wa  Israel  , Marekani  inatambua  kuwa  ni  kinyume na  sheria  ujenzi  wa  makaazi  hayo, lakini  makaazi  hayo yameendelea  kuongezeka  na  kupanuka   katika  wakati wa  kila  serikali  ya  Israel  tangu  kuanza  kwa  uvamizi huo  Juni 1967.

Katika  muda  wa  miezi  michache   baada  ya  Israel kuyakamata  maeneo  kadha  ya  Waarabu  katika  vita  vya siku  sita  vya  ukingo  wa  magharibi  na  ukanda  wa Gaza  pamoja  na  Jerusalem  ya  mashariki,  ardhi ambayo  hivi  sasa  inatarajiwa  kuundwa  taifa  la Wapalestina , kazi  ilianza   katika  ujenzi  wa  makaazi  ya kwanza   ya  Gush Etzion, karibu  na  Jerusalem.

Viongozi  wa  harakati  za  walowezi  wa  Kiyahudi wanaliona  eneo  la  ukingo  wa  magharibi  na  Jerusalem ya  mashariki  kuwa  ni  sehemu  ya  taifa  la  Israel , ambayo  wamepewa  Wayahudi   na  Mungu,  na wanaviona  vitongoji  hivyo  vya  walowezi  kuwa  ni  hali halisi  katika  maeneo  hayo  kuweza  kuzuwia kuondolewa.

Tangu  pale  zilipofanyika   hatua  za   kuleta  amani  za mjini  Oslo  mwaka  1993, idadi  ya  walowezi  imeongezeka kwa  karibu   mara  tatu  kwa  kuhamasishwa   na  viongozi wa  Kiyahudi  wenye  msimamo , ikiwa  ni  pamoja  na waziri  mkuu  Benjamin  Netanyahu  na  waziri  mkuu  wa zamani  Ariel  Sharon , ambaye  ni  maarufu  kama,  "baba wa  harakati  za  walowezi". Akizungumzia  mkutano uliofanyika  huko  Sharm el  Sheikh  nchini  Misri, rais  wa Israel Shimon  Perez  alionyesha  matumaini  kuhusu mikutano  hiyo.

Kikao  cha  jana  mjini Sharm el Sheikh  kilikuwa  bora zaidi  kuliko  watu  wote  waliokuwa  na  shaka  na  wasio na  matumaini  walivyotarajia. Siamini  kuwa  unaweza kutatua  matatizo  haya   kwa  mikutano  miwili  au  mitatu, lakini  ulikuwa  mwanzo  mzuri  na  kuna  hali  ya kuendelea. Na  hisia  zangu  nilipozungumza  na  waziri mkuu  wetu  mkuu  pamoja  na  viongozi  wengine , ni kwamba  kuna  hisia  kuwa  tufanye  kile  kinachowezekana kwa  ajili  ya  hali  bora  ya  pande  zote  zinazohusika.

Waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Marekani  Hillary Clinton  amewaunga  mkono  viongozi  wa  Israel  na Palestina  leo  kabla  ya  mazungumzo  yao  yanayojaribu kuvunja  mkwamo  kuhusiana  na  ujenzi  wa  vitongoji hivyo  vya  walowezi  katika  maeneo  yanayokaliwa   kwa nguvu  na  Israel  ya  ukingo  wa  magharibi.

Huu  ndio  wakati,  na  hawa  ndio  viongozi, amesema Clinton  kabla  ya  kuonana  na  waziri  mkuu  Benjamin Netanyahu  na  rais  Mahmoud  Abbas, ambao  wameanza tena   mazungumzo  yao  ya  moja  kwa  moja   ya  kutafuta amani  wiki  mbili  zilizopita   baada  ya  kutokufanyika  kwa muda  wa   miezi  20.

Mwandishi : Sekione  Kitojo / RTRE / AFPE

Mhariri : Mohammed  Abdul Rahman