1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MECCA : Mamilioni ya Waislamu waanza hija leo

28 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCfk

Waislamu milioni mbili leo hii wanaanza ibada ya hija mjini Mecca Saudi Arabia huku hatua za usalama zikiwa zimeongezeka kuzuwiya makanyagano ambao kila mwaka husababisha vifo kadhaa.

Hija hiyo inaanza leo kwa waumini kukusanyika mjini Mina na alfajiri ya kesho Ijumaa wataanza kuelekea kwenye Mlima Arafat ambapo watatumia siku hiyo kuomba msamaha kwa Mwenyeenzimungu.

Baadae mahujaji watarudi Mina kuchinja mnyama ambaye kawaida huwa ni kondoo kwa ajili ya Eid al Adha hapo Jumamosi siku ambayo pia inajulikana kwa Waislamu kuwa nsi Sikuu ya Idd el Hajj.

Mahujaji hao pia watatumia siku mbili nyengine wakiwa hapo kwa ajili ya ibada ya kupiga mawe shetani ambayo ni ishara ya kumkana shetani.

Hija hiyo ambayo inamalizika Jumatatu ni mojawapo ya nguzi tano za Uislamu na ni wajibu kutimizwa na Waisalemu wote wenye uwezo angalau mara moja katika umri wa uhai wao.