1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 10 baada ya Saddam Hussein

Sekione Kitojo
29 Desemba 2016

Dikteta  wa Iraq  aliyeondolewa madarakani Saddam Hussein alinyongwa  ndani  ya  vituo  vya utawala  wake vya mateso muongo  mmoja uliopita hapo Desemba 30, 2006.

https://p.dw.com/p/2V1Le
Saddam Hussein vor Gericht
Saddam Hussein akiwa mahakamani Picha: David Furst/AFP/Getty Images

Desemba  30, 2006, Saddam  alionyongwa  katika  makao makuu  ya  idara  ya  upelelezi  katika  jeshi  katika  wilaya ya  Kadhimiyah  kaskazini  mwa  Baghdad. Maafisa  ambao walishuhudia  kuuwawa  kwa  Saddam Hussein  aliyekuwa na  umri  wa  miaka  69  mapema  alfajiri, aliendelea  kuwa mkaidi  hadi  mwisho  wake,  akipambana  na  maadui zake  wa  Iran  na  Marekani  na  kuwasifu  wapiganaji ambao  wameipeleka  Iraq  katika  ukingo  wa  vita  vya wenywe  kwa  wenyewe.

"Sikuona  hata  chembe  ya  hofu," mshauri  wa  zamani wa  usalama  wa  taifa  Mowaffak al-Rubaie, ambaye aliratibu   hatua  ya  kunyongwa, aliliambia  shirika  la habari  la  AFP  mwaka  2013.

Mowaffak al-Rubaie
Mowaffak al-RubaiePicha: SABAH ARAR/AFP/Getty Images

"Sikusikia  hali  yoyote  ya  kujuta kutoka  kwake, sikusikia ombi lolote la  msamaha  kutoka  kwa  Mungu .. ama  ombi la  kusamehewa," alisema.

Rubaie  alisema  alivuta  ubao  kumnyonga  Saddam, lakini hakuna  kilichotokea. Mtu  ambaye  hakutambuliwa  kisha alivuta  ubao  huo  kwa  mara  ya  pili, na  kumuua.

Muda  mfupi  kabla  ya  kuuwawa , Saddam alianza kusoma dua , lakini  hakuweza  kuimaliza. 

Saddam Husseins Grabmahl in al-Audscha
Kaburi la Saddam Hussein katika kijiji cha Ajda karibu na TrikritPicha: DW/B. Svensson

Vidio  ya  dakika  mbili  na  nusu  iliyochukuliwa  kwa  njia ya  simu  ya  mkono  ilimuonesha  akianguka  kupitia  katika mlango  wa  chini  ya  ardhi  na  kufariki  huku  kukiwa  na shangwe  kutoka  kwa  watu  waliokuwapo.

Picha  iliyoonesha kwa  karibu  ilionesha  kichwa  chake kikielemea  upande  mmoja  katika  kitanzi, na  shingo yake  ikiwa  imekatika.

Mtu  huyo  aliyekuwa  na  madaraka makubwa  aliuwawa baada  ya  kupatikana  na  hatia  ya  uhalifu  dhidi  ya ubinadamu kwa  mauaji  ya  mwaka  1982  ya  watu  148 washia  katika  mji  wa  Dujail. Mauji  hayo  yanafuatia jaribio  la  kuuwawa  dhidi  yake  katika  eneo  hilo.

Utawala  wa kikandamizaji

Utawala  wake  uligubikwa  na  ukandamizaji  wa  kinyama , vita  na  vikwazo  vilivyoumiza  vya  kimataifa.

Saddam Hussein Statue
Sanamu la Saddam Hussein Picha: SABAH ARAR/AFP/Getty Images

Saddam  alipinga uhalali  wa  mahakama  maalum  ya  Iraq iliyoundwa  kwa  msaada  wa  marekani  kumshitaki, na kuieleza  kesi  yake  iliyofanyika  kuanzia  Oktoba  2005 hadi  Julai  2006  kuwa  ni  "dhihaka".

Baadhi  ya  Waislamu  wa  madhehebu  ya  Shia  , ambao waliteseka  katika  utawala  wake, walicheza  mitaani baada  ya  kunyongwa. Lakini  kuuwawa  huko, ambapo Marekani  ilisema  haikushiriki , kulilaaniwa  na  Wairaq  wa madhehebu  ya  Sunni   na  serikali  kadhaa  duniani -- licha  ya  sio  na  mahasimu  wakubwa  wa  Saddam Hussein Israel  na  Iran.

Siku  moja  baada  ya  kunyongwa, Saddam  alizikwa katika  kijiji  cha  Awja, alikozaliwa  karibu  na  Tikrit , kilometa  160 kaskazini  mwa  baghdad.

Raghad Hussein 2007
Mwanae Saddam Hussein , Raghda Hussein akihudhuria katika sala ya maombi kwa baba yake nchini YemenPicha: AFP/Getty Images

Ilikuwa  pia  karibu  na  Tikrit  ambapo  katika  usiku  ambao haukuwa  na  mbalamwezi  Desemba  13, 2003, dikteta huyo  wa  zamani  alikamatwa  na  majeshi  ya  Marekani. Washington  ilitoa  kiasi  cha  dola  milioni  25  kama zawadi  kwa  mtu  atakayetoa  taarifa  za  kukamatwa kwake.

Baada  ya  kupinduliwa  na  majeshi  ya  uvamizi  ya Marekani , Saddam Hussein  alikimbia  kwa  muda  wa miezi  minane  kwa  msaada  wa  walinzi  wake  wa  karibu kutoka  katika  familia  yake, kwa  mujibu  wa  viongozi  wa kikabila  wa  eneo  hilo.

Lakini  mmoja  alimsaliti, na  kuwaelekeza  wanajeshi  wa Marekani  kufika  katika  maficho  yake  baada  ya  yeye binafsi  kukamatwa. Tofauti  kabisa  na  maisha  ya  kifahari katika   jumba  la  rais , Saddam  alipatikana  amejificha katika  shamba  katika  kile  ambacho  wanajeshi  wa Marekani  walikiita "tundu  la  panya" , maficho  ya  chini  ya ardhi  ambapo  kuna  nafasi  ndogo  kwa  ajili  ya  mtu mmoja  kujilaza ,  akiwa  na  vifaa  vya  kujipatia  hewa  na feni  ya  kumpepea. 

Mwandishi: Sekione  Kitojo /  Afpe

Mhariri: Grace Patricia Kabogo