1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo mwishoni mwa wiki

27 Oktoba 2008

Young Africans yailaza Simba 1:0 katika Ligi ya Tanzania. Hoffeinheim yaparamia kileleni mwa Bundesliga.

https://p.dw.com/p/Fhvt
Chinedu Obasi wa Hoffenheim atia mabao 2.Picha: AP

Young Africans ya Tanzania yavunja mwiko wa miaka 7 wa kutotamba mbele ya mahasimu wao Simba,FCLiverpool yaipiku Chelsea na kuparamia kileleni mwa Premier-League-ligi ya Uingereza.Hoffenheim, klabu iliopanda daraja ya kwanza msimu huu imeizaba Hamburg mabao 3-0 na kuparamia kileleni mwa Bundesliga.

Baada ya Kaiserslauten msimu wa 1998-99 kutoka daraja ya pili ya Bundesliga na kutawazwa mabingwa wa daraja ya kwanza msimu huo huo, Hoffenheim klabu iliopanda msimu huu, yaonesha yataka kuiigiza Kiaserslauten. Hoffenheim jana iliitundua kileleni Hamburg-waliokua viongozi wa ligi kwa kuwachapa mabao 3-0. Hamburg haikuwa na jibu la mchezo wa kasi wa washambulizi wa Hoffenheim pale mabao 2 ya Chinedu Obasi na 1 la Ivesevic, yalipokamilisha msangao mkubwa katika Bundesliga. Kwa pigo hilo,Hamburg iliteleza nafasi ya 3 ya ngazi ya ligi kutoka ya kwanza ikiwa na jumla ya pointi 17 kwa 19 za Hoffenheim.Hivyo, Hamburg ina pointi 1 zaidi kuliko Stuttgart iliangukia nafasi ya 4.

Kocha wa chipukizi Hoffenheim, Ralf Rangnick ameelezea ufunguo wa ushindi wa hoffenheim jana dhidi ya Hamburg:

"Tumeendeleza mchezo mzuri wa mechi iliopita.Kutokana na mchezo wetu nyumbani uliopita dhidi ya B .Dortmund iliocheza katika kombe la ulaya la UEFA ,tulijua kwamba hali ni sawa na ile ya mchezo uliopita kwavile, Hamburg nayo ilicheza alhamisi katika kombe la UEFA."

Ilikua kukumbusha tu wachezaji wetu kucheza kama vile na kuongeza kasi mchezo."Bayer Leverkusen iliotamba kwa mabao 2-0 hapo ijumaa dhidi ya FC Cologne, iko nafasi ya pili.Stuttgart iliikomea Buchum jana mabao 2-0 na sasa imeitangulia Bayern Munich kwa pointi 1.

Mabingwa Munich wamenyakua ushindi wao 3 wiki hii ,kwani walitoka nyuma hapo jumamosi na kufuta mabao 2 ya Wolfsburg na mwishoe, wakashinda kwa mabao 4-2.Kocha wa Munich, Jurgen Klinsmann anaanza kuvuta pumzi baada ya jahazi lake kwenda mrama.

PREMIER LEAGUE:

Katika Premier-League-ligi ya Uingereza, FC Liverpool jana ilitamba mbele ya Chelsea kwa bao 1:0 huko Stamford Bridge.Pigo hilo lilimaliza rekodi ya Chelsea ya kutofungwa nyumbani katika mechi 86.Alonso ndie alielifumania lango la Chelsea kwa bao hjilo pekee hapo jana.Liverpool sasa ina pointi 23 kwa 20 za Chelsea kama Hull City.Arsenasl imeangukia nafasi ya 4 baada ya kuikandika West Ham United mabao 2:0.

OLYMPIQUE MARSEILLE imekosa jana nafasi ya kuparamia kileleni mwa Ligi ya Ufaransa (Ligue I ) baada ya kulazwa na Paris st.Germain kwa mabao 4-2.Hilo ni pigo la kwanza la Marseille msimu huu.Katika mpambano wake uliopita wa Champions League ,Olympique Marseille,ilitandikwa mabao 2-0 na PSV Eindhoven .Sasa wako nafasi ya pili kutoka kileleni -pointi 2 nyuma ya Olympic Lyon waliomudu sare tu ya 0:0 na Auxerre hapo jumamosi.

Ama katika la Liga-Ligi ya Spian , Valencia imeteleza kidogo na uongozi wao kileleni umepunguzwa hadi pointi 1 .Hii ilifuatia bao la David Villa la kusawazisha katika mpambano na Huelva .Villareal imeangukia sasa nafasi ya 4 katika La Liga ikiwa na pointi 18.Kwanzwa walifuta mabao 2 na halafu kuongoza kwa mabao 4-2 na mwishoe, wakamalizana sare 4:4 na Atletico Madrid.

Katika Serie A, ligi ya Itali -Inter Milan,mabingwa wamebakia wakiongoza Ligi lakini pamoja na Udinese kufuatia kutoka sare 0:0 na Genoa.Udinese ina pointi 17 kama Milan .Udinese imeichapa As Roma mabao 3-1.Napoli ni timu ya tatu yenye pointi 17 kama Inter na Udinese.

Nchini Holland,PSV Eindhoven, walipata pigo lao la pili tena mfululizo waliporaruliwa kwa mabao 3-2 na Roda Kerkrade na sasa wamerudi nyuma nafasi ya 6 wakiwa na pointi 12.Groningen,wameichapa Sparta Rotterdam mabao 3-0.

Nchini Ureno, mabingwa FC Porto walishindwa kwa mara ya kwanza msimu huu na jirani zao Leixoes walipochapwa mabao 3-2 hapo jumamosi.Sasa Leixoes ina pointi sawa na Porto.Benefica Lisbon, imeipiku pia Porto kutokana na ushindi wao wa mabao 2-1 dhidi ya Naval .

Huko Afrika Mashariki, mwishoni mwa wiki ,mahasimu 2 wa jadi walipimana nguvu : Simba sports club na Young Africans.Ingawa Young Africans ikiongoza Ligi ya Tanzania-bara kitambo sasa na kuiacha nyuma Simba, mpambano wa jumamosi katika uwanja mkuu wa Taifa ,jini Dar-es-salaam, haukuwa na uhakika wa ushindi kwa Younga. Swala likawa je, Younga ingevunja mwimko wa kushindwa kutamba mbele ya Simba kwa kiasi cha miaka 7 ?

Jibu la Younga lilikuwa itaweezekana na firimbi ya mwisho ilipolia, Younga iliwazima simba kunguruma kwa bao 1:0 .