1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo wiki hii

18 Julai 2008

Kombe la klabu bingwa Afrika laanza kwa changamoto kati ya al Ahly na zamalek mjini Cairo.

https://p.dw.com/p/EepI

Kombe la klabu bingwa barani Afrika linarudi uwanjani mwishoni mwa wiki huku Zamalek ikiumana na Al Alhly mjini Cairo,Dynamo ya zimbabwe ikiwa na miadi ASEC Abidjan,Al Hilal na Enyimba na mabingwa wa Kamerun Contonsport Garoua wakiwa na miadi na TP Mazembe ya Jamhuri ya kidemokrasi ya kongo.

Mjini Dar-es-salaam na Morogoro, kinaendelea mwishoni mwa wiki hii pia kinyan'ganyiro cha kuania nafasi za robo-finali za kombe la kagame-kombe la klabu bingwa-kanda ya Afrika mashariki na kati.

Kuwasili kati ya wiki hii kwa Ronaldinho wa Brazil mjini Milan,Itali kuichezea AC Milan kumewatia hamasa mashabiki na kuongeza ununuzi wa tiketi za Serie A.

FIFA inazungumza na Brazil juu ya uwezekano wa kuchukua jukumu la kuandaa kombe la dunia 2010 endapo Afrika kusini, itashindwa-hii ni kwa muujibu wa gazeti la Spian.Na Spain yenyewe yamkini ikanyan'ganyia na Uingereza tiketi ya kuandaa kombe la dunia 2018.

Katika kombe la klabu bingwa kanda ya Afrika Mashariki na kati mjini Dar-es-salaam na Morogoro kuania tiketi za robo-finali, hatima ya mabingwa wa tetezi kutoka Rwanda APR kurudi Kigali na kombe iko hatarini.Kwani, mabingwa hao walichapwa juzi mabao 3:1 na Miembeni ambayo jumamosi inacheza na Simba.

Firimbi italia kesho katika Uwanja wa Cairo,Misri, pale mabingwa mara kadhaa wa Afrika-Al Ahly ya Misri itakapoumana na Zamalek pia ya Misri.

Changamoto hii ya kukata na shoka kati ya "Mashetani wekundu na "White Knights" hapo kesho ndio kilele cha mapambano 4 ya mwishoni mwa wiki hii ya awamu ya makundi mbali mbali ya timu zinazoania kombe la klabu bingwa ikianza:

Mbali na zahama hiyo kati ya Al Ahly na zamalek mjini Cairo, Dynamos ya zimbabwe inaikaribisha ASEC Abidjan ya ivory Coast katika kundi A huku Al-Hilal ya Sudan inajiwinda kutamba nyumbani mbele ya Enyimba ya Nigeria .

Contonsport Garoua ya Kamerun ni wenyeji wa TP Mazembe ya Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo katika kundi B.

Washindi wa kila kundi A na B na timu itayomaliza wapili,

zitasonga mbele hadi nusu-finali iotakayochezwa kwa mfumo wa nyumbani na ugenini.Mabingwa mwishoe watatoroka na kitita cha dala milioni 1 na kukata tiketi ya kombe la klabu bingwa za dunia linaloandaliwa na FIFA kila mwaka huko Tokyo,Japan.

Macho ya mashabiki wa dimba barani Afrika yanakodolewa kuona iwapo mara hii tena kama mwaka jana, timu za afrika ya kaskazini zitatamba mbele ya zile za kusini mwa Jangwa la sahara:

Miezi 2 iliopita mabingwa Etoile du sahel ya Tunisia ,walikuwa miongoni mwa klabu zilizokiona kilichomtoa kanga manyoya miongoni mwa timu hizo kali za Afrika kaskazini.Mwaka jana klabu 7 kati ya 8 ziliozounda Ligi ndogo zilitoka Afrika kaskazini ,mwaka huu lakini ni mbili tu zilizovuka salama hadi hatua hii.Timu za afrika magharibi,Afrika ya kati,Mashariki na hata kusini bado zinaania kombe.

Mara hii yaonesha mabingwa si chini ya mara 5 Al Ahly waweza kutamba tena lakini kitisho kwao kinatoka kwa Enyimba .Hatahivyo, haifai kuzitoa maanani Zamalek na ASEC ,kwani zaweza pia kutamba.

Kwa ufupi, timu zote 4 pamoja na TP Mazembe zimetawazwa mabingwa hapo kabla .Al Ahly imetwa mara 5 kombe hili kama vile Zamalek .Enyimba na Mazembe kila moja imetoroka na kombe mara 2 huku ASEC ikiwamabingw amara 1.

Dynamo ya zimbabwe iliwasili finali 1998 na Al Hilal walitolewa nusu-finali mwaka jana na mabinghwa etoile du sahel.Cotonsport ya kamerun ni mwanagenzi katika kundi hilo ,lakini mambo yaweza nayo yakabadilika na upepo ukavumia upande wao .

kwani Contonsport punde hivi wametoroka na taji lao la 5 la mfululizo la ubingwa nchini kamerun na waweza pia kuondoka na vikombe vyote 2 nyumbani kwani wameingia finali ya kombe la taifa.

Hata Al Ahly na Zamalek zilipepesuka karibuni ,kwani mastadi wao 2-Emad Moteab wa al ahly na amr Zaki wa zamalek wamehiyari kucheza katika premier League,Uingereza kuliko kubakia Misri.

Moteab amefunga mkataba wa miaka 3 na Bristol City inayocheza daraja ya pili ya premier League na Zaki alietamba mapema mwaka huu katika kombe la Afrika la mataifa, anahamia Wigan Athletics.

Nje ya dimba la klabu bingwa barani Afrika, taarifa kutoka Spain, mabingwa wa Ulaya zadai kuwa, FIFA inazungumza na Brazil kuwa tayari kuandaa kombe lijalo la dunia 2010 endapo Afrika kusini,itashindwa kuandaa kombe hilo la kwanza kabisa barani Afrika .Gazeti la michezo la Spian AS limeripoti kati ya wiki hii kwamba nchi moja ya Amerika kusini iliochaguliwa kuandaa kombe la dunia 2014,imekuwa ya kwanza kuulizwa kujitwika jukumu hilo endapo Afrika kusini ikikwama.AS haikutaja chanzo chake cha habari.

Gazeti likaongeza kuwa FIFA-shirikisho la dimba ulimwenguni limeiarifu serikali ya Afrika kusini uamuzi huo wa kushauriana na shirikisho la dimba la Brazil.

Hatahivyo, waandazi wa kombe la dunia nchini Afrika kusini wana yakini kwamba wataweza kuliandaa ,licha ya kuchelewa ujenzi wa baadhi ya viwanja.Rais wa FIFA Sepp Blatter,aliungama mwezi uliopita kwamba ana mpango B endapo Afrika kusini ikiteleza.

Spain iliotawazwa mabingwa wa Ulaya mwezi uliopita huenda wakanyan'ganyia na Uingereza nafasi ya kuandaa kombe hilo la dunia 2018-vyombo vya habari vya Spian vimeripoti.Ni Uingereza tu hadi sasa ilioomba kuandaa kombe la dunia mwaka huo.

Ronaldinho,mwanasoka bora wa dunia kabla kaka,wote kutoka Brazil aliwasili Milan kati ya wiki hii na kupokewa kwa shangwe na shamra shamra na mashabiki.

Kuwasili kwa mbrazil huyo katika serie A-Ligi ya Itali kumechangia kununuliwa kwa wingi kwa tiketi za msimu mpya kutoka mashabiki wa AC Milan.

Ronaldinho amejiunga na AC Milan kutoka FC Barcelona ambako alicheza na stadi wa Kamerun Samuel Eto'o.

Na Eto'o nae asemekana anatakiwa na klabu ya Tashkent, huko Kazakhstan kwa kitita cha dala milioni 40.

Nae stadi wa kiungo wa afrika Kusini Quinton Fortune anasakwa kama udi na ambari na klabu ya portsmouth na Ipswich.Stadi huyo wa zamani wa Manchester united anatafuta sasa klabu mpya kuhamia.Fortune aliruhusiwa kuiacha klabu yake ya Bolton mwishoni mwa msimu uliopita.