1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Holbrooke Afghanistan

Oumilkher Hamidou16 Februari 2009

Mkakati mpya wa Marekani kuelekea Afghanistan.

https://p.dw.com/p/GvA9
Richard Holbrooke azungumza na rais Karsai wa AfghanistanPicha: AP


Uhusiano kati ya Afghanistan na Marekani unazidi kupooza.Rais Hamid Karsai hajawahi hata mara moja kupigiana simu na kiongozi mwenzake wa Marekani Barack Obama.Bila ya msaada wa Marekani,Karzai asingeweza hata chembe kuingia madarakani.Hivi sasa lakini yadhihirika kana kwamba siku zake madarakani zakurubia kumalizika.Agosti 20 rais mpya atachaguliwa nchini Afghanistan.Mjumbe maalum wa Marekani nchini Afghanistan,Richard Holbrooke,akiwa ziarani mjini Kaboul mwishoni mwa wiki (february 14 na 15),amezungumza sio tuu na Hamid Karzai,bali pia na wanasiasa wen gine wanaoweza kutetea wadhifa huo.


Ingawa rais wa Afghanistan alionana na Richard Holbrooke,muda mfupi kabla ya kuondoka Kaboul,hata hivyo mjumbe huyo maalum wa Marekani walizungumza kwa pamoja na waandishi wa habari.Bado kwa hivyo utawala mpya wa Marekani haujampa kisogo "mlindwa" wa rais wa zamani George W. Bush.Shughuli za kubuni mkakati mpya wa Marekani kuelekea Afghanistan,si bado hazijamalizika.


Kuulizwa maoni yake serikali ya Afghanistan juu ya mkakati huo mpya ni hatua ya kutuliza mambo.Na hata sauti  Karsai anayozidi kuipaza dhidi ya nchi za magharibi itabidi kupunguzwa.


Ni mkuki unaokata kuwili kwa Karzai,kwamba jeshi la Afghanistan linahusishwa sana katika maandalizi na utekelezaji wa hujuma za Marekani dhidi ya Wataliban na al-Qaida.Raia wa kawaida wanapouwawa kufuatia hujuma hizo,na yeye pia analaumiwa.


Hadi wakati huu,lawama zake dhidi ya idadi kubwa ya wahanga zilimfanya ajiweke kando na wamarekani,japo  kama tangu zamani amekua akiangaliwa na wengi kua ni kibaraka cha Marekani.


Haijulikani lakini bado kama Karzai ataweza kujivunia uungaji mkono wa utawala mpya wa Marekani,uchaguzi utakapoitishwa nchini mwake msimu wa kiangazi ujao.Richard Holbrooke alizungumza pia na wagombea wengine wa kiti cha uraia mjini Kaboul.Mjini Washington viongozi wanashuku kama Karzai ndie kiongozi atakaeleta maedeleo ya kweli nchini mwake.Anakosolewa kuchangia katika maafa yaliyoko.Anaangaliwa kama mtu asiyekua na msimamo,si kiongozi jasiri.


Hakuna anaeamini kama Hamid Karsai atafanikiwa kubadilisha mkondo wa mambo na kuimarisha shughuli za serikali yake kuweza kupiga vita mitindo ya kupendeleana ,rushwa na biashara ya madawa ya kulevya.


Bila shaka rais Karsai habebi peke yake dhamana ya maafa yanayoikaba Afghanistan.Wanajeshi karibu 70 elfu wa kigeni wamewekwa nchini humo.Hata hivyo waasi wanazidi kupata nguvu.Idadi ya mashambulio imeongezeka mwaka jana,na wanamgambo wa Talivban na Al Qaida wanazidi kuingia Afghanistan wakitokea Pakistan.


Marekani,mfadhili mkubwa wa miradi ya kijamii nchini Afghanistan na nchi yenye kuchangia wanajeshi wengi zaidi,inataka kuamua hivi sasa jinsi ya kuendelea na jukumu lake katika nchi hiyo.Kama wanajeshi wengi zaidi watahitajika ili kuwashinda nguvu magaidi,kama mfumo mpya wa utawala na uchumi unaonawiri  ndio njia na kama Karsai ni msaada au kizingiti.


Rais Barack Obama anatazamiwa kufafanua mkakati wake kuhusu Afghanistan wakati wa mkutano wa kilele wa jumuia ya kujihami ya NATO ,April mwaka huu,hadi wakati huo kuna muda wa kutosha wa kujaribu kukitegua kitandawili hicho.