1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Motlanthe anakabiliwa na mtihani mkubwa

Kalyango Siraj26 Septemba 2008

Wa kwanza ni kukiunganisha tena chama cha ANC

https://p.dw.com/p/FPUp
Rais Motlanthe. Ana mtihani mkubwaPicha: AP

Rais mpya wa Afrika Kusini Kgalema Motlanthe anakabiliwa na changamoto kubwa za kisiasa pamoja na kiuchumi.Na inaonekana kama hana mda wa kutosha kuweza kukabiliana na changamoto hizo.

Kgalema Motlanthe aliechaguliwa na kutawazwa jana kama rais wa tatu wa Afrika Kusini iliohuru licha ya kuushangiliwa sana bungeni baada ya kuchaguliwa lakini ana mitihani mingi inayomkabili kutokana na yale ambayo ameyarithi.

Kutokana na mda alionao wa miezi sita au tano hivi kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu mwakani yaani Aprili mwaka wa 2009.

Mtihani wake wa kwanza katika muda huo mfupi, ni kuondoa mgawanyiko mkubwa kuwahi kukimba chama tawala cha African National Congress ANC.Kwa kuwa anafahamika kama mpenda amani na kuheshimiwa sana katika chama hicho kilichogawanyika,huenda akawa mtu muafaka kwa kibarua hicho.

Lakini mchambuzi wa masuala ya kisiasa kutoka Chuo Kikuu cha Rhodes,Steven Friedman amemuonya kuwa ni lazima achunge kwani anaweza akaangaliwa kwa jicho baya kutoka kwa wafuasi wa kiongozi wa chama cha ANC Jacob Zuma,ikiwa atafanikiwa katika kibarua hicho na kujipatia sifa .

Zuma anatarajiwa rais wa nchi hiyo mwaka ujao na mvutano wake na Mbeki umepelekea Mbeki kung'atuka.

Yeye mshauri katika kampuni ya utafiti ya Executive Research Associates,Nel Marais anasema kuwa ni lazima Motlanthe awe muangalifu ili asije akampiku Zuma kwani anajua kuwa ni rais wa mda.

Wachambuzi wamekariri kuwa kuendeleza sera za kiuchumi za Mbeki ndio nguzo muhimu ya kurejesha imani miongoni mwa wawekezaji ambayo imevurugwa na mgogoro wa kisiasa.

Kwa upande mwingine Motlanthe atakuwa chini ya shinikizo la wafuasi wa Zuma wenye kuegemea mrengo wa kushoto wakimtaka abadili sera kuwasaidia watu maskini walio wengi ambao hadi sasa hawajafaidika na utawala wa wazalendo weusi.

Dhana ya kuwa Mbeki alishindwa kuwahudumia wazalendo hao ndio sababu kuu ya kuporomoka kwake ndani ya chama kilichomrithisha na Zuma kama kiongozi wake mwezi Disemba.

Kuhusu changamoto za kiuchumi lakujiuliza ni ikiwa matatizo ya Afrika Kusini yatasubiri hadi mwakani kuweza kuleta sera za mageuzi.

Mfumuko wa bei umepanda sana kuliko ilivyokuwa kabla ya kumalizika mfumo wa kibaguzi.Kiwango cha kukua kwa uchumi kimekuwa kidogo na mgogoro wa umeme nao tena umeathiri machimbo ya madini ya dhahabu na madini ya Platinum.

Katika hotuba yake ya kwanza Motlanthe amekariri kuendeleza kile kilichokuwepo na kudhihirisha hilo amewateuwa tena mawaziri kadhaa waliokuwa katika serikali ya Bw Mbeki.Miongoni mwao ni waziri wa fedha Trevor Manuel.Kujiuzulu kwa waziri huyo mapema wiki hii,kama sehemu ya mawaziri walio watiifu kwa Mbeki kulitikisa masoko, hadi alipotoa tangazo kuwa yuko tayari kufanya kazi chini ya rais yeyote atakaechaguliwa.