1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hugh Masekela baba wa Jazz Afrika Kusini afariki dunia

Amina Mjahid
23 Januari 2018

Mwanamuziki wa Jazz Afrika Kusini na Kimataifa Hugh Masekela amefariki dunia akiwa na miaka 78. Masekela alisifika kwa nyimbo zake na mchango wake katika harakati za kupinga ubaguzi wa rangi.

https://p.dw.com/p/2rNZu
Hugh Masekela
Picha: Imago/R. Gigler

Familia ya Hugh Masekela msanii maarufu kwa kupuliza tarumbeta, ilisema katika taarifa kwamba baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na maradhi ya saratani ya tezi dume, msanii huyo aliaga dunia mjini Johannesburg. Taarifa hiyo ilimsifia Masekela baba wa muziki wa Jazz Afrika kusini kwa mchango wake mkubwa kimziki uliyobakia ndani ya mioyo na kumbukumbu za mamilioni ya watu.

Kwa upande wake rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amemsifia Masekela kama msanii wa muziki wa  jazz, mpiga tarumbeta maarufu, mwanaharakati wa utamaduni na mtu aliyekuwa katika harakati za ukombozi. "Aliuweka hai mwanga wa uhuru duniani kote katika harakati zake za kupinga ubaguzi wa rangi kupitia muziki wake na kushinikiza uungwaji mkono wa kimataifa, fani ya muziki na nchi kwa Ujumla tumempoteza mtu muhimu sana," alisema rais Jacob Zuma.

Hugh Masekela
Hugh Masekel baba wa muziki wa jazzPicha: DW/König

Muimbaji mmoja wa Afrika Kusini Johnny Clegg alimuelezea Masekela kama mwanamuziki bora na siku zote akiishi kwa mitazamo ya asili yake ya Afrika Kusini, aliondoka Afrika Kusini wakati ilipoongozwa na watu weupe mwaka wa 1960 na hakurejea hadi pale Nelson Mandela alipoachiwa huru mwaka wa 1990.

Muda wote alikuwa uhamishoni mjini London.  Baadaye alihamia mjini New York Marekani na kukutana na msanii mwenzake wa Afrika Kusini Miriam Makeba, Dizzy Gillespie na Harry Belafonte. Masekhela na Makeba waliishi maisha ya ndoa ya muda mfupi na Miriam Makeba.

Miongoni mwa nyimbo zake zilizovuma na zilizopendwa ni ile ya "Bring Him Back Home", Akishinikiza Nelson Mandela achiwe huru. Hugh Masekela alitumbuiza katika hafla ya ufunguzi wa fainali za kombe la dunia za mwaka 2010 zilizofanyika nchini Afrika Kusini ikiwa ni mara ya kwanza fainali hizo kufanyika barani Afrika. Aidha Waziri wa sanaa nchini Afrika Kusini Nathi Mthethwa amesema leo kwamba taifa hilo limempoteza mwanamuziki wa haiba ya kipekee aliburudisha nyoyo za watu wa taifa hilo kupitia miziki yake.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFP

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman