1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Abdelhamid Abaaoud ameuawa katika msako wa Saint-Denis

19 Novemba 2015

Mtuhumiwa mkuu wa mashambulizi ya Paris, Abdelhamid Abaaoud, ni miongoni mwa watu waliouawa katika msako mkubwa wa polisi uliofanyika kwenye kitongoji kimoja kaskazini mwa mji mkuu wa Ufaransa, Paris.

https://p.dw.com/p/1H8mX
Mshukiwa mkuu wa mashambulizi ya Paris, Abdelhamid Abaaoud
Mshukiwa mkuu wa mashambulizi ya Paris, Abdelhamid AbaaoudPicha: picture-alliance/dpa/Dabiq

Mwendesha mashtaka mkuu wa Ufaransa, Francois Molins amethibitisha leo kuwa mwili wa Abaaoud ulikutwa ukiwa na majeraha mengi, baada ya msako huo uliosababisha kiasi ya watu wawili kuuawa, akiwemo mwanamke mmoja anayedhaniwa kujilipua kwa kujitoa mhanga.

Molins amesema Abaaoud mwanamgambo wa kundi lenye itikadi kali la Dola la Kiislamu-IS, raia wa Ubelgiji mwenye umri wa miaka 28, anatuhumiwa kupanga mashambulizi ya Paris usiku wa Ijumaa iliyopita yaliyowaua watu 129 na kuwajeruhi wengine 352.

Awali polisi walidhani Abaaoud yuko Syria, lakini upelelezi wao uliwaongoza kwenye nyumba moja mjini Paris katika kitongoji cha Saint-Denis na maafisa wa jeshi waliokuwa na silaha nzito waliivamia nyumba hiyo kabla ya kuiharibu kabisa.

Uchunguzi wa kutambua alama za vidole umetumika kuutambua mwili wa mtuhumiwa huyo mkuu, ambaye mwili wake umepatikana kwenye kifusi cha jengo lililovamiwa na vikosi vya usalama na kushambuliwa kwa risasi na mabomu.

Waziri Mkuu apongeza

Waziri Mkuu wa Ufaransa, Manuel Valls amepongeza hatua ya vikosi vya usalama vya Ufaransa kwa kufanikisha mauaji ya Abaaoud, baada ya kufanya msako mkubwa mjini Paris.

''Wengi wenu tayari mnajua, lakini nashukuru operesheni iliyofanyika jana. Mwendesha mashtaka mkuu wa Ufaransa amethibitsha kwamba sasa tunajua Abaaoud, aliyepanga mashambulizi, ni miongoni mwa waliouawa katika msako wa vikosi vya usalama,'' alisema Valls.

Valls ameonya kuna hatari huenda IS wakatumia silaha za sumu au vijidudu dhidi ya Ufaransa, na kusema kuna haja ya kuchukua tahadhari iwapo chochote kitatokea.

Aidha wabunge wa Ufaransa wameidhinisha kurefushwa kwa muda wa hali ya hatari nchini humo kwa kipindi cha miezi mitatu, pamoja na kuidhinisha kufungwa mitandao kama kuna haja ya serikali kufanya hivyo katika kipindi hicho.

Maafisa wa kijeshi wa Urusi na Ufaransa wakutana

Waziri Mkuu wa Ufaransa, Manuel Valls
Waziri Mkuu wa Ufaransa, Manuel VallsPicha: Getty Images/T. Chesnot

Wakati huo huo, mkuu wa majeshi wa Urusi, Jenerali Valery Gerasimov na mwenzake wa Ufaransa Jenerali Pierre de Villiers wamefanya mazungumzo kwa njia ya simu hii leo, ambapo wamejadiliana kuhusu ushirikiano wa kijeshi na hatua za kuchukua dhidi ya magaidi wa IS nchini Syria.

Aidha, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Uhispania, Jorge Fernandez Diaz amesema Abaaoud alijaribu kuwapatia mafunzo ya kigaidi wanawake wanaoishi Uhispani kupitia mitandao ya kijamii, ili waweze kujiunga na IS.

Kwa upande wake Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel ameitaka jumuiya ya kimataifa kusimama pamoja katika mapambano dhidi ya ugaidi. Wito huo ameutoa leo mjini Berlin wakati akizungumza na kiongozi mwenzake wa Austria, Werner Faymann.

Yote hayo yanajiri wakati wakati ambapo jeshi la muungano wa kimataifa linaloongozwa na Marekani likiwa limefanya mashambulizi 19 ya anga dhidi ya IS nchini Iraq hapo jana, karibu na Kirkuk, Kisik, Mosul, Ramadi na Sinjar. Marekani imesema jeshi hilo pia limefanya mashambulizi manane ya anga dhidi ya IS nchini Syria.

Kansela Angela Merkel
Kansela Angela MerkelPicha: Reuters/S. Stache

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/RTRE,AFPE,DPAE,APE
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman