1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mukwege arudishiwa ulinzi wa Umoja wa Mataifa

10 Septemba 2020

Wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa wameanza tena kumlinda mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Denis Mukwege

https://p.dw.com/p/3iGIk
Demokratische Republik Kongo Bukavu | Demis Mukwege erhält Friedensnobelpreis
Picha: picture-alliance/AP Photo/Norwegian Church Aid

Vitisho hivyo alivyopokea Mukwege ambaye ni daktari wa wanawake vilisababisha maandamano na wito wa kimataifa wa kutaka apewe ulinzi. Tangu alipoponea shambulizi nyumbani kwake mwaka 2012 ambapo mlinzi wake aliuwawa, daktari huyo amekuwa akiishi katika hospitali ya Panzi karibu na mji wa Bukavu. Hospitali hiyo inawashughulikia wanawake waliobakwa katika mikoa jirani.

Meneja wa mawasiliano wa Mukwege anasema vikosi vya Umoja wa Mataifa viliondoka katika hospitali hiyo mnamo mwezi Mei kutokana na mripuko wa virusi vya corona akidai hakukuwa na ulinzi kabisa tangu wakati huo.

Msemaji wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa nchini Kongo, MONUSCO amelithibitishia shirika la habari la Ufaransa AFP kuwa ulinzi katika hospitali hiyo ulikuwa umeondolewa.

Demokratische Republik Kongo | Überfall auf UN-Lager in Beni
Walinda amani wa Umoja wa Mataifa CongoPicha: Reuters/File Photo/O. Oleksandr

Ila umoja huo sasa umesema ipo haja ya daktari huyo kupewa ulinzi baada ya kupokea vitisho pamoja na familia yake kupitia mitandao ya kijamii. Hii ni baada ya shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu la Amnesty International juma lililopita kuitaka serikali ya Kongo na Umoja wa Mataifa kuchukua hatua za kumlinda.

Soma pia:Asasi za kiraia DRC zalaani vitisho dhidi ya Mukwege

Katika ujumbe aliouandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, Mukwege mwenyewe ameushukuru Umoja wa Mataifa kwa kutuma kikosi cha MONUSCO katika hospitali ya Panzi kwa ajili ya ulinzi wa wagonjwa na wahudumu katika hospitali hiyo.

Wiki iliyopita mamia ya watu wakiwemo wanawake aliowatibu waliandamana mjini Bukavu pamoja na mji mkuu, Kinshasa wakitaka daktari huyo kulindwa. Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Stephan Dujarric amesema umoja huo unaendelea kufanya kazi pamoja na Mukwege na serikali ya Kongo.

Mbali na kazi yake kama daktari wa wanawake, Mukwege amekuwa akifanya kampeni za kutaka adhabu itolewe kwa waliotekeleza ukiukaji wa haki za binadamu katika vita vya Kongo vya kati ya 1996 – 1998 na 1998 – 2003. Madhara ya vita hivyo bado yanaliathiri eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.

afp