1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MUNICH : Marekani yashangazwa na matamshi ya Putin

11 Februari 2007
https://p.dw.com/p/CCTK

Rais Vladimir Putin wa Urusi katika mashambulizi makali kabisa dhidi ya Marekani kuwahi kuyatowa katika kipindi cha miaka saba madarakani ameishutumu Marekani hapo jana kwa kujaribu kuiburuza dunia.

Ikulu ya Marekani imesema imeshangazwa na kusikitishwa na shutuma hizo za Putin lakini imeongeza kusema kwamba itaendelea kushirikiana na Urusi katika fani kama vile za kupiga vita ugaidi na kupunguza kuenea pamoja na tishio la silaha za maangamizi makubwa.

Putin ametumia hotoba yake katika mkutano wa usalama wa kimataifa mjini Munich Ujerumani kuishutumu Marekani kwa kutumia nafasi ya kuwa taifa pekee lenye nguvu kubwa duniani kuchochea mashindano mapya ya kutengeneza silaha duniani. Putin amesema kuendelea kwa Marekani kutumia nguvu za kijeshi kumekuwa kukiyashajiisha mataifa madogo kutengeneza silaha za nuklea.

Ikulu ya Marekani imesema shutuma hizo za Putin sio sahihi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ameutaka Umoja wa Kujihami wa Mataifa ya Magharibi NATO na Umoja wa Ulaya kushirikiana nchini Afghanistan dhidi ya kuibuka upya kwa kundi la Taliban.