1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali ya Maldives yaelezwa kuwa shambulio dhidi ya demokrasia

Amina Mjahid
9 Februari 2018

Televisheni inayoegemea upande wa upinzani katika visiwa vya Maldives imejifungia yenyewe kufuatia visitisho kwa wafanyakazi wake huku serikali ikiendelea na kamata kamata dhidi ya upinzani.

https://p.dw.com/p/2sObc
Maledivischer Präsident Yameen Abdul Gayoom
Picha: picture-alliance/M.Sharuhaan

Maafisa katika kituo hicho cha televisheni cha Raajje wamesema vitisho kwa wafanyakazi wake kuhusu namna wanavyoripoti taarifa juu ya mgogoro wa kisiasa katika visiwa hivy vilivyoko katika Bahari ya Hindi, imewalazimu kusimamisha kwa muda matangazo yake.

"Kituo hicho kimepokea vitisho kutoka kwa wabunge wa serikali na wengine,” alisema mbunge mmoja wa upinzani Eva Abdulla.

Proteste der Opposition auf den Malediven
Maafisa wa polisi katika visiwa vya Maldives wakiwa tayari kudhibiti maandamano ya upinzani Picha: Reuters

Visiwa vya Maldives kiliingia katika mzozo wa kisiasa wiki hii wakati rais Abdulla Yameen alipotangaza sheria ya hali ya hatari na kuamru kukamatwa kwa majaji waliyoruhusu kuachiwa kwa wapinzani wake.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amemhimiza rais huyo kuondoa sheria hiyo ya hali ya hatari, huku Mkuu wa haki za binaadamu katika Umoja wa Mataifa Zeid Ra'ad Al Hussein akieelezea hatua za rais Abdulla Yameen kama shambulizi dhidi ya demokrasia ya Maldives.

Hapo jana afisa mmoja mkuu wa Umoja wa Mataifa alitoa onya kwa Baraza la Usalama la Umoja huo kwamba hali katika eneo hilo sio nzuri na huenda ikawa mbaya zaidi.

Maandamano mpaka sasa yemedhibitiwa lakini upinzani pamoja na chama tawala wamewatolea mwito wafuasi wao kwa maandamno baada ya sala ya Ijumaa.

Rais Yameen ambaye amekuwa akiwaweka korokoroni wanasiasa wa upinzani tangu alipoingia madarakani mwaka wa 2013 amekataa shinikizo kutoka Jamii ya Kimataifa juu ya mgogoro katika visiwa hivyo. Awali alikataa kukutana na wanadiplomasia kutoka Umoja wa Ulaya, Ujerumani na Uingereza waliosafiri katika visiwa hivyo vya utalii kwa mazungumzo naye.

Malediven, Demonstranten der maledivischen Opposition rufen Parolen, die während eines Protestes die Freilassung politischer Gefangener fordern
Baadhi ya waandamanaji katika visiwa vya Maldives wanaotaka wanasiasa wa upinzani waliyokamatwa waachiwe huruPicha: picture-alliance/M.Sharuhaan

China, India na serikali nyengine za Magharibi wamewataka raia wao wasisafiri kuelekea nchini humo wakati huu wa mgogoro wa kisiasa.

Huku hayo yakiarifiwa Rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa India Narendra Modi pia wamepaza sauti zao juu ya hili na kuelezea wasiwasi wao kuhusu mzozo wa kisiasa katika visiwa vya Maldives. Viongozi wote wawili wamesisitiza umuhimu wa kuheshimu taasisi zinazofanya kazi zake kidemokrasia na pia kuheshimu utawala wa sheria.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFP/dpa

Mhariri: Grace Patricia Kabogo