1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaArmenia

Mzozo wa Nagorno-Karabakh wafika mahakama ya haki, ICJ

Tatu Karema
12 Oktoba 2023

Armenia imewataka majaji wa mahakama ya ICJ kuilazimisha Azerbaijan kuondoa wanajeshi wake jimbo la Nagorno - Karabakh.

https://p.dw.com/p/4XRte
Armenia imetoa ombi kwa mahakama ya ICJ kuiamuru Azerbaijan kuwaondoa wanajeshi wake na maafisa wa usalama kutoka kwa taasisi zote za kiraia katika eneo la Nagorno-Karabakh.
Armenia imetoa ombi kwa mahakama ya ICJ kuiamuru Azerbaijan kuwaondoa wanajeshi wake na maafisa wa usalama kutoka kwa taasisi zote za kiraia katika eneo la Nagorno-Karabakh.Picha: Wiebe Kiestra/UN

Armenia na Azerbaijan zimekabiliana katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ siku ya Alhamisi, huku Armenia ikiwataka majaji wa mahakama hiyo kuilazimisha Azerbaijan kuondoa wanajeshi wake kutoka jimbo lililojitenga la Nagorno - Karabakh na kuwaruhusu Waarmenia waliotoroka kutoka eneo hilo kurejea kwa usalama. 

Armenia imetoa ombi kwa mahakama ya ICJ kuiamuru Azerbaijan kuwaondoa wanajeshi wake na maafisa wa usalama kutoka kwa taasisi zote za kiraia katika eneo la Nagorno-Karabakh.

Pia imeitaka mahakama hiyo kuhakikisha kuwa Azerbaijan inajiepusha kuchukuwa hatua zozote ambazo huenda zikawa na athari zitakazosababisha Waarmenia waliobakia katika eneo hilo la Karabakh kupoteza makazi yao ama kuzuia kurejea kwa haraka na kwa usalama kwa wakimbizi wa eneo hilo.

Bunge la Armenia laidhinisha nchi hiyo kujiunga na ICC

Kikao cha Alhamisi, cha kesi hiyo ndicho cha hivi karibuni zaidi katika mvutano wa muda mrefu wa kisheria kati ya mataifa hayo mawili hasimu.

Kila nchi inaishtumu nyingine kwa kukiuka Mkataba wa Kimataifa wa Kutokomeza Aina Zote za Ubaguzi wa Rangi (ICERD).

Azerbaijan ilichukuwa udhibiti wa eneo hilo linalozozaniwa la Ngorno -Karabakh kwa mara ya kwanza katika muda wa miongo mitatu.
Azerbaijan ilichukuwa udhibiti wa eneo hilo linalozozaniwa la Ngorno -Karabakh kwa mara ya kwanza katika muda wa miongo mitatu.Picha: AZIZ KARIMOV/REUTERS

Uwezo wa mahakama ya ICJ

Mahakama ya ICJ hufanya maamuzi kuhusu mizozo baina ya mataifa lakini ingawa maamuzi yake yanafungamanisha kisheria, haina uwezo wa kuyatekeleza.

Kesi hiyo katika mahakama ya ICJ inakuja wiki chache tu baada ya shambulio kubwa la Azerbaijan ili kuchukuwa udhibiti wa eneo hilo linalozozaniwa la Ngorno -Karabakh kwa mara ya kwanza katika muda wa miongo mitatu.

Uturuki, Azerbaijan zasusia mkutano wa Ulaya kuhusu mvutano wa Karabakh

Operesheni hiyo ya siku moja ilisababisha kutoroka kwa idadi kubwa ya Waarmenia, huku wengi wao wanaokadiriwa kuwa takriban 120,000 wakikimbilia Armenia.

Baada ya operesheni hiyo ya kijeshi, Armenia iliilaumu Azerbaijan kwa kufanya operesheni ya utakasaji wa kikabila ili kuwafurusha Waarmenia wote katika eneo la Nagorno-Karabakh.

Azerbaijan yakanusha madai dhidi yake

Lakini Azerbaijan imekanusha vikali madai hayo na kutoa wito hadharani kwa Waarmenia katika eneo hilo la Karabakh kuendelea kuishi katika eneo hilo na kujumuishwa tena na Azerbaijan.

Mamlaka katika jimbo hilo la Nagorno Karabakh ilitangaza kwamba serikali yake itavunjwa kufikia Januari 1 mwakani.
Mamlaka katika jimbo hilo la Nagorno Karabakh ilitangaza kwamba serikali yake itavunjwa kufikia Januari 1 mwakani.Picha: DAVID GHAHRAMANYAN/REUTERS

Watu 85,000 wakimbilia Armenia kutoka Nagorno-Karabakh

Pia kufuatia operesheni hiyo, wabunge wa Armenia waliidhinisha hatua muhimu ya kujiunga na mahakama nyingine ya kimataifa yenye makao yake makuu mjini The Hague, Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).

Hatua hii iliikasirisha Urusi, mshirika wa jadi wa Armenia kwasababu ilikuwa imetoa agizo la kukamatwa kwa rais wa nchi hiyo Vladimir Putin kwa madai ya kuwateka nyara watoto wakati wa uvamizi wake nchini Ukraine.

Urusi kujadili mustakabali wa amani Nagorno-Karabakh

Eneo la milima la Nagorno Karabakh, lilikuwa na idadi kubwa ya Waarmenia lakini linatambuliwa kimataifa kuwa sehemu ya Azerbaijan tangu kuanguka kwa uliokuwa Muungano wa Kisovieti.

Waarmenia katika eneo hilo walijitangazia uhuru wao kwa msaada wa Armenia wakati wa kuvunjika kwa Muungano wa Kisovieti mnamo mwaka 1991.