1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nakba - "maafa" ya Wapalestina

Zainab Aziz
15 Mei 2018

Maafa makubwa yaliwafika Waarabu kutokana na kuundwa taifa la Israel mwaka 1948. Leo Wapalestina wanaombeleza siku hiyo wanayoiita Nakba

https://p.dw.com/p/2xk5w
Naqba Nakba Palästina Gedenkfeier Gedenken Vertreibung
Picha: AP

Miaka 30 kabla la hapo yaani  tarehe 2 mwezi Novemba mwaka wa 1917 waziri wa mambo ya nje wa Uingereza Arthur James Balfour alimwandikia rais wa shirikisho la Wayahudi la nchini Uingereza Lionel Walter Rothschild kumwambia kwamba Uingereza itatumia nguvu zote kuunda taifa la Wayahudi. Kabla ya hapo idadi kubwa ya wayahudi kutoka nchi za Ulaya Mashariki walikuwa wanakimbia maangamizi. Watu hao walihamia Palestina.

Kati ya mwaka 1882 na 1939 Wayahudi 389,000  walihamia Palestina lakini wakati huo tayari walikuwapo watu 450,000 waliokuwa wanaishi kwenye eneo hilo na asilimia 90 walikuwa ni Waarabu. Ni kutokana na hali hiyo kwamba Waarabu walihisi kutishiwa na kuanzia mwaka 1920 ujio wa Wayahudi ulisababisha mivutano na jamii hizo mbili zilianza kukabiliana

Baada ya mwaka 1945 Manazi nchini Ujerumani walikuwa tayari wameshawaangamiza Wayahudi milioni sita. Uingereza iliuomba Umoja wa Mataifa mnamo  mwaka 1947 kuigawanya Palestina. Asilimia 57 ilikuwa sehemu ya Wayahudi  na asilimia 43 ilikuwa ya Waarabu.

Tarehe 14 mwezi Mei mnamo mwaka 1948 waziri mkuu wa serikali ya mpito ya Israel David Ben Gurion alitangaza taifa  jipya la Israel. Muda mfupi baada ya tangazo hilo wayahudi na Waarabu waliingia vitani. Nchi za Kiarabu ziliwaunga mkono Wapalestina. Vita hivyo vilikuwa maafa kwa Waarabu.

Wakimbizi wa Kipalestina mnamo mwaka 1948
Wakimbizi wa Kipalestina mnamo mwaka 1948Picha: picture-alliance/CPA Media

Maalfu kwa maalfu walilazimika kuondoka kwenye sehemu zilizokaliwa na Israel. Watu zaidi ya 700,000 walikimbia na athari zake bado hazijaondoka kwani mgogoro kati ya Israel na Wapalestina  bado  haujatatuliwa  hadi leo. Pande mbili hizo zimepigana vita mara kadhaa, ikiwa pamoja na vile vita vya siku sita vya mnamo mwaka 1967.

Wakimbizi wa Kipalestina waliondikishwa rasmi wanaishi kwenye kambi zinazotambuliwa nchini Jordan,Lebanon Syria na kwenye ukingo wa magharibi na Jerusalema mashariki. Wengi waliondoka Palestina na funguo za nyumba  zao. Watu hao waliondoka na matumaini ya kurejea  nyumbani siku moja. Watu hao waliondoka na watoto wao na sasa watoto hao pia wana watoto na hivyo kuifanya idadi ya Wapalestina hao kufikia milioni tano. Mtaalamu wa masuala ya Mashariki ya Kati  Marlene Schneiper anasema katika kitabu chake kinachoitwa Nakba kwamba idadi ya wakimbizi  hao inazidi kuongezeka.

Baada ya vita vya mwaka 1967 Israel ilianza kujenga makaazi ya walowezi kwenye ukingo wa magharibi. Mgogoro Kati ya Wayahudi na Wapalestina mpaka sasa umeshadumu miaka 70. Msomi Hanan Ashrawi mwanasiasa mkongwe na aliyekuwa mjumbe wa baraza la Wapalestina amesisitiza kuhusu juhudi za kuushughulikia mgogoro kati ya Israel na Wapalestina.

Msomi Hannan Ashrawi mwanasiasa mkongwe wa Palestina
Msomi Hannan Ashrawi mwanasiasa mkongwe wa PalestinaPicha: Hanan Ashrawi

Bi Ashrawi amesema Wapaletiana wamo kwenye machungu na wakati mtu unapokabiliwa na machungu na taharuki hawezi kukaa mahala pamoja tu na kuangalia kwa macho bilaya kufanya chochote, bila shaka atatumia kitu chochote kilicho mbele ya macho yake. hali ya Gaza na Ukingo wa Magharibi inabidi iingiliwe kati kwa maana ya kuokoa amani inayotoweka kila uchao.

Kwa mara nyingine Wapalestina wanashiriki katika harakati za kudai haki ya wakimbizi wa Kipalestiana ya kurejea katika nchi yao. Maalfu wameandamana karibu na mpaka wa Israel kupinga maafa yaliyotokana na kuundwa taifa la Israel miaka 70 iliyopita, kadhia hiyo inatwa Nakba na Wapalestina.

Mwandishi: Zainab Aziz/Knipp/DW

Mhariri: Iddi Ssessanga