1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nani atakuwa rais mpya wa FIFA?

25 Februari 2016

Ijumaa mjini Zurich vyama vya mataifa 209 wanachama wa shirikisho la kandanda duniani FIFA vitapiga kura kumchagua rais wa shirikisho hilo

https://p.dw.com/p/1I2Q5
FIFA Bewerber

Nafasi inayoachwa wazi na Sepp Blatter ambaye amezuiwa na kamati ya maadili ya shirikisho hilo kujihusisha na michezo kwa muda wa miaka minane.

Gianni Infantino na Sheikh Salman bin Ebrahim al Khalifa wanaongoza mbio hizo za kuwania kuwa rais wa FIFA, lakini uchunguzi wa maoni uliofanywa na shirika la habari la AFP kutoka kwa wanachama wa shirika hilo linaloongoza kandanda duniani unaonesha mbinu tata za kisiasa na hali ya sintofahamu inazunguka uchaguzi wa leo.hirika la AFP limewasiliana na vyama vya mataifa 209 katika shirikisho hilo linalokumbwa na matatizo katika soka duniani na kuwauliza ni nani kati ya wagombea hao watano wanaomuunga mkono kuchukua nafasi ya Sepp Blatter.

FIFA Kongress Zürich Hallenstadion
Ukumbi utakaoandaa mkutano wa FIFAPicha: picture-alliance/dpa/P.Seeger

Baadhi walitoa jibu na kisha wakabadili msimamo wao. Baadhi wamesema hawana uhakika watampigia nani kura. Kuwait na Indonesia bila shaka hazitapiga kura kwa kuwa zimezuiwa na FIFA.

Kwa jumla , vyama 161, ama asilimia 77 ya vyama , vimejibu uchunguzi huo wa maoni , vikitoa ishara ya kushangaza ya nia yao ya wapi watapiga kura.

Licha ya juhudi kadhaa, hakuna aliyejibu simu katika chama cha soka nchini China. Afisa mmoja alijibu simu katika shirikisho la soka la Korea kaskazini lakini ilisema kura ni siri.

Mashirika 68 yametangaza kumuunga mkono Infantino , ambaye amejiunga na mbio hizo baada ya kiongozi wake wa shirikisho la kandanda barani Ulaya UEFA Michel Platini alilazimishwa kujitoa , na wengine 28 wamejiegemeza kwa Sheikh Salman, rais wa shirikisho la kandanda barani Asia.

Mwanya uliopo katika uungaji mkono kati ya wagombea hao wawili unapaswa pia kuangaliwa kwa tahadhari. Vyama katika bara la Ulaya vimeelekezwa kumuunga mkono Infantino na chama cha UEFA walikuwa tayari zaidi kufuata mwelekeo huo kuliko vyama kutoka Asia na Afrika ambavyo vimejitokeza kumuunga mkono Sheikh Salman.

Schweiz suspendierter FIFA-Präsident Sepp Blatter
Rais anayeondoka wa FIFA Sepp BlatterPicha: picture-alliance/dpa/W. Bieri

Ni vyama vinne tu vimejitokeza hadharani na kusema vinamuunga mkono Mwanamfalme Ali Bin al Hussein, makamu wa zamani wa rais wa FIFA kutoka Jordan. Kikisi chake cha kampeni kinamatumaini ya kupata zaidi ya kura hizo nne.

Hakuna aliyejitokeza wazi na kuahidi kupiga kura kwa wagombea wawili walionaki katika uchaguzi wa kesho mjini Zurich - Jerome Champagne wa Ufaransa na Tokyo Sexwale kutoka Afrika kusini. Kwa jumla vyama 61 vimekataa kutangaza wazi mwelekeo wa kura zao katika uchaguzi huo utakaompata kiongozi atakayeliongoza shirikisho hilo la kandanda lililozongwa na kashfa tele katika enzi za Sepp Blatter.

Idadi hiyo ya juu inaashiria hoteli za kifahari mjini Zurich zinazopendelewa na wajumbe wa FIFA zilitapakaa hali ya ushawishi , njama na majadiliano ya usiku kucha kuelekea uamuzi utakaofanyika hii leo huku baadhi ya mashirika yakijaribu kupuuzia maelekezo ya vyama vyao vikuu vya kikanda. Mashirika manne kati ya sita yameelekeza wanachama wao kupiga kura kwa mgombea mmoja.

Infantino raia wa Uswisi , mwenye asili ya Italia ana ungwa mkono na UEFA kwa kura 53, shirikisho la vyama vya kandanda Amerika ya kusini lenye kura 10, na wajumbe saba wa shirikisho la kandanda la America ya kati, ambalo ni sehemu ya kundi kumbwa la kanda ya shirikisho la CONCACAF kwa ajili ya Amerika ya kaskazini na kati.

Kwa mujibu wa mtazamo huo atapata kura 70. Sheikh Salman mwelekeo wake ni tofauti. Anaungwa mkono na vyama kutoka Asia na Afrika ambavyo kwa jumla vina kura 100.

Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe
Mhariri: Mohammed Khelef