1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

"Ni rahisi kuzishinikiza nchi za kidemokrasi"

Maja Dreyer25 Julai 2007

Baada ya wauguzi wa Bulgaria na daktari mmoja kuwasili barani Ulaya na kuachiliwa huru, kisa hicho leo hii kinatathminiwa na wahariri.

https://p.dw.com/p/CHSJ

Basi maoni yao ni yapi? La kwanza hilo hapa gazeti la “Landshuter Zeitung”:

“Baada ya miaka minane kifungoni na hofu ya kutolewa adhabu ya kifo, kesi hiyo ambayo mara nyingine imeonekana kuwa ni mchezo mbaya wa tamthilia imemalizika. Kwa bahati mbaya, mtungaji wa mchezo huu hakuadhibiwa bali anasifiwa. Kiongozi huyu wa Libya Muaamar el Ghaddafi lakini angepaswa kuimaliza kesi hiyo mapema. Hatimaye, nchi za Ulaya zimelipa fedha nyingi. Siku hizi basi ni rahisi kuyashinikiza mataifa ya kidemokrasia ya Magharibi. Faida ni kubwa.”

Malalamiko haya yanaandikwa katika “Landshuter Zeitung”. Mhariri wa “Süddeutsche Zeitung” anachambua maslahi ya Muammar el Ghaddafi na kusema kiongozi huyu anahitaji fedha:

“Ghaddafi anategemea kuwa na mafanikio kwa sababu uchumi wa nchi yake umekwama na hawezi kuwaridhisha wananchi wake kwa muda mrefu zaidi. Inambidi kuwekeza katika sekta ya mafuta. Hivi karibuni, Tony Blair, pia aliitembelea Libya kwenye ziara yake ya mwisho kama waziri mkuu wa Uingereza. Hapo walikubaliana juu ya biashara kubwa ambayo inaipa kampuni ya Uingereza BP haki ya kuchimba mafuta nchini Libya.”

Tukibakia kwake Ghaddafi, tumasoma vile mhariri wa “Frankfurter Rundschau” anavyokasirika juu ya matokeo ya Libya:

“Wanasiasa wanasema haiwezekani kuzishinikiza nchi za kidemokrasi. Lakini hali halisi ni kwamba: Ndiyo, inawezekana. Ikiwa ni kuhusu maisha ya binadamu, serikali hizo hazina chaguo lingine ila tu kulipa yale yanayotakiwa. Kesi hiyo ya Libya inaonyesha kwamba si tu makundi ya wahalifu au magaidi, bali pia ni serikali pamoja na mfumo wao wa kisheria ambazo zinatumia vibaya msimamo wa thamani ya maisha ya binadamu.”

Leo hii, kama tulivyosikia katika matangazo, rais Sarkozy wa Ufaransa anaitembelea Libya. Sarkozy pia anasifiwa kwa msaada wake katika kupatanisha juu ya kesi ya wauguzi wa Bulgaria. Wahariri wa humu nchini lakini wana wasiwasi juu ya sera za rais huyu wa Ufaransa. Kuhusiana na hayo, mhariri wa “Weser-Kurier” ameandika:

“Ni wazi kwamba Ulaya inaitegemea Libya kama mtoaji wa nishati, kama mshirika katika vita dhidi ya ugaidi na katika kukabilana na idadi kubwa ya Waafrika wanaokimbilia Ulaya. Sera hizo ni kali lakini zinahitajika. Msimamo wa nchi za Ulaya ni kwamba rais Sarkozy wa Ufaransa anafaa kuwa na jukumu kubwa, lakini asiwe ni mwongozaji katika sera za pamoja.”