1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nini kitatokea iwapo Ukraine itajiunga na NATO?

Josephat Charo
6 Julai 2023

Ukraine inaendelea na juhudi zake za kujiunga na jumuiya ya kujihami ya NATO, huku muungao huo wa kijeshi ukijiandaa kufanya mkutano wake wa kilele wiki ijayo mjini Vilnius nchini Lithuania.

https://p.dw.com/p/4TVII
Russland Ukraine Krieg NATO
Picha: Ukrainian Presidential Press Office/AP/picture alliance

Ukraine iliongeza juhudi zake za kutaka kujiunga na jumuiya ya kujihami NATO baada ya uvamizi wa Urusi mwaka uliopita, ikihoji kwamba ahadi za kuhakikishiwa usalama ilizopewa kutoka kwa Urusi, Marekani na Uingereza wakati ilipozikabidhi silaha zake za nyuklia kwa Urusi mnamo mwaka 1994 hazikuwa na maana yoyote. Swali linaulizwa, kipi kitakachotokea kama Ukraine itajiunga na NATO.

Huku nchi za Ulaya mashariki zikisema aina fulani ya mpango unaotoa ramani ya uanachama unatakiwa kuwasilishwa kwa Ukraine katika mkutano wa kilele wa jumuiya ya NATO mjini Vilnius siku ya Jumanne na Jumatano wiki ijayo, Marekani na Ujerumani bado zinasita kuchukua hatua yoyote ambayo huenda ikausogeza muungano huo wa kijeshi karibu na kuingia vitani na Urusi.

Rais wa Urusi Vladimir Putin ametaja utanuzi wa NATO kuelekea Urusi katika kipindi cha miongo miwili iliyopita kama ufunguo muhimu ya uamuzi wake wa kuwapeleka maalfu ya vikosi vya wanajeshi katika nchi jirani ya Ukraine mnamo Februari 24 mwaka 2022.

Utanuzi wowote wa NATO sharti ukubaliwe na nchi zote 31 wanachama na katibu mkuu wa jumuiya hiyo Jens Stoltenberg tayari ameshafutilia mbali kuialika rasmi Ukraine katika mkutano huo wa Vilnius.

Russland Ukraine Krieg NATO
Katibu mkuu wa NATO Jens Stoltenberg, wa pili kushoto, na Rais wa Ukraine Volodymyr zelenskiy, kulia, wakizungumza wakati wa mkutano wao mjini Kyiv, Ukraine, Aprili 20, 2023.Picha: Ukrainian Presidential Press Office/AP/picture alliance

Kuna hatua kadhaa ambazo Ukraine imeshazichukua kuelekea uanachama wa NATO, na uwezekano wa muafaka kuhusu hatua zitakazofuata na mtazamo wa Urusi kuhusu matukio haya.

Soma pia:Katibu mkuu wa NATO kubakia madarakani kwa mwaka mwingine

Mnamo mwaka 2008 NATO ilikubali katika mkutano wake wa mjini Bucharest kwamba Ukraine, ambayo ilikuwa sehemu ya muungano wa zamani wa Sovieti mpaka uliposambaratika 1991, huenda hatimaye ikajiunga na NATO.

Lakini viongozi wa NATO hawakuipa Ukraine hati inayoainisha mpango wa kuileta karibu na jumuiya hiyo. Baadaye Urusi ikaiteka rasi ya Crimea mnamo 2014 na ikaviunga mkono vita vya waasi wanaopigania kujitenga mashariki mwa Ukraine.

Chini ya mchakato wa Mpango wa uanachama wa NATO uliofuatwa na nchi za zamani za kikomunisti za Ulaya Mashariki, nchi zinazotaka kuwa wanachama sharti zidhihirishe kwamba zinakidhi vigezo vya kisiasa, kiuchumi na kijeshi na zinaweza kuchangia kijeshi kwa operesheni za jumuiya ya NATO.

Tangia 1999, nchi nyngi zinazonuia kujiunga na NATO zimeshiriki mchakato huo, ingawa utaratibu huu si wa lazima. Finland na Sweden ambazo zamani zilikuwa nchi ambazo hazikuegemea upande wowote, zilialikwa kujiunga moja kwa moja na jumuiya hiyo.

Mataifa makuu NATO yataka mchakato uwekwe kando

Haijabainika wazi jinsi njia ya Ukraine itakavyokuwa kuelekea uanachama wake wa NATO, na nchi nyingi zaidi, ikiwemo Uingereza na Ujerumani, zinapendekeza mchakato wa mpango wa uanachama uwekwe kando.

Soma pia: NATO yajadili hakikisho la usalama wa Ukraine baada ya vita

Kupitia hatua hii, NATO yumkini ikashughulikia madai ya Ukraine na washirika wake wa Ulaya Mashariki kwenda mbali zaidi ya lugha iliyotumika katika makubalino ya mkutano wa Bucharest mnamo 2008 bila kuipa Ukraine mualiko halisi wala ratiba ya tarehe.

NATO yajadili jinsi ya kuipatia Ukraine silaha zaidi

Jeshi la Ukraine limechukua hatua kubwa kuelekea viwango vya NATO tangu uvamizi kamili wa Urusi. Mchakato unashika kasi huku silaza na risasi zake zilizotengenezwa enzi ya Sovieti zikiisha pole pole na huku nchi za Magharibi zikiwapa mafunzo vikosi vya wanajeshi wake kulingana na viwango vya NATO na kutuma silaha za kisasa zaidi na zaidi.

Kipengee muhimu cha kuisaidia Ukraine kipo katika msingi wa sheria ya NATO, muungano ulioasisiwa mnamo 1949 kwa lengo la kukabiliana na kitisho cha mashambulizi ya Sovieti katika ardhi ya nchi wanachama.

Soma pia: NATO yaapa kuiunga mkono Ukraine bila kuchoka

Kinatajwa kuwa mojawapo ya sababu kubwa kwa nini Ukraine haiwezi kujiunga na NATO huku ikiwa katika mgogoro na Urusi, kwa kuwa hatua hii huenda kwa haraka ikautumbukiza muungano huo katika vita halisi.

Kipengee hicho, Ibara ya 5 ya Mkataba wa Washington, kinasema shambulizi dhidi ya mshirika mmoja linachukuliwa kuwa shambulizi kwa washirika wote.

Stoltenberg ameshasema wazi kwamba huku NATO ikilazimika kujadili uwezekano wa kuipa Ukraine hakikisho la usalama kwa wakati baada ya vita, ahadi za usalama chini ya kipengee hicho zitatolewa tu kwa wanachama kamili wa jumuiya hiyo.

Urusi imesema kutatokea matatizo kwa miaka mingi ijayo ikiwa Ukraine itajiunga na NATO na imetahadharisha juu ya hatua ambazo haikuziweka wazi bayana za kujibu ili kujihakikishia usalama wake.

Chanzo: rtre