1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Nini kinafuata kwa Marekani-India baada ya njama ya mauaji?

1 Desemba 2023

Waendesha mashtaka wa Marekani wamedai afisa mmoja wa India alikuwa nyuma ya njama ya kumuua mwanaharakati wa Sikh huko New York. Je, ni nini athari zake kwa mahusiano ya Marekani na India?

https://p.dw.com/p/4Ze8v
Picha za Sikh Toronto
Thuma mpya dhidi ya India zimesababisha ulinganisho na kifo cha mwanaharakati wa Sikh Hardeep Singh Nijjar nchini Canada.Picha: Khalid Eid/DW

Jambo jipya, lakini la kushangaza linatikisa uhusiano kati ya India na Marekani - Waendesha mashtaka wa Marekani wamemshtaki raia wa India kwa kupanga mauaji ya raia wa Marekani mjini New York.

Nyaraka za mahakama ya Marekani zinadai afisa wa serikali ya India alimkodi Nikhil G., raia wa India, kumuua mfuasi maarufu wa Sikh. Mlengwa anaripotiwa kuwa mwanaharakati wa Sikh Gurpatwant Singh Pannun. Nikhil G. alikamatwa msimu huu wa joto katika Jamhuri ya Czech.

Ufichuzi huo umekuja miezi miwili baada ya Waziri Mkuu wa Canada Justin Trudeau kuishutumu India kwa kuhusika katika mauaji ya mwanaharakati mwingine wa Sikh, Hardeep Singh Nijjar, mwezi Juni - madai ambayo India imeyakanusha na kuitaka Ottawa kuonyesha ushahidi. Matamshi ya Trudeau yamesababisha mzozo wa kidiplomasia unaoendelea kati ya Ottawa na New Delhi.

Gurpatwant Singh Pannun ni nani?

Mtu anaedaiwa kuwa mlengwa wa njama hiyo ya New York ni raia wa Marekani na Canada aliyezaliwa Punjab. Ni mshauri mkuu wa shirika la Sikhs for Justice, ambalo linaunga mkono kujitenga kwa jimbo la Punjab kutoka India.

Kanada I Nach Mord an Sikh-Aktivist
Wanaharakati wa Sikh wakiandama mbele ya ubalozi wa India Canada kupinga mauaji yanayodaiwa kuagizwa na serikali ya India dhidi ya viongozi wa wanaotaka kujitenga.Picha: Ines Pohl/DW

Shirika la kupambana na ugaidi nchini India hivi karibuni lilifungua kesi dhidi ya Pannun, kwa madai kwamba alitumia jumbe za video kwenye mitandao ya kijamii mapema mwezi Novemba kuwaonya abiria wa Air India kwamba maisha yao yako hatarini.

Soma pia: Watu 41 walionasa ardhini kwa waki mbili India wako mbioni kuokolewa

Pannun alipuuzilia mbali kesi dhidi yake akiitaja kuwa "isiyo na maana" na kuliambia shirika la habari la Reuters kwamba alikuwa akiwahimiza watu kususia shirika hilo la ndege na "siyo kulilipua".

Waendesha mashtaka wamesema raia wa India Nikhil G. alikodiwa na afisa aliyetajwa kama CC-1. Wizara ya Sheria ya Marekani ilisema CC-1 ni mfanyakazi wa wakala wa serikali ya India ambaye amejieleza kama "afisa mkuu wa nyanjani" mwenye majukumu katika "usimamizi wa usalama" na ujasusi. Hapo awali alihudumu katika Jeshi kuu la Polisi la Akiba, ilisema wizara.

Kisha Nikhil G. alifika kwa mtu ambaye aliamini kuwa ni mshirika wa kihalifu ili kusaidia kukodisha muuaji kwa ajili ya mauaji ya Pannun. Lakini mshirika aliyewasiliana naye alikuwa wakala wa siri wa idara ya Udhibiti wa Madawa ya kulevya ya Marekani.

Kulingana na Wizara ya Sheria ya Marekani, Nikhil G. alitoa maoni yake kuhusu mauaji ya Nijjar mwezi Juni akisema kulikuwa na "walengwa wengi" na hakukuwa na haja ya kusubiri.

Majibu kutoka Washington na New Delhi

Majibu ya India kuhusu kisa hiki cha karibuni zaidi yamekuwa ya tahadhari zaidi kuliko majibu yake kwa shutuma za Canada. Hata kabla ya mashtaka kuwasilishwa, Wizara ya Mambo ya Nje ya India ilisema New Delhi ilikuwa imepokea baadhi ya taarifa za usalama kutoka Marekani na kuanzisha "kamati ya juu ya uchunguzi kuchunguza mambo yote muhimu ya suala hilo." Taarifa hiyo haikumtaja Pannun.

Ushoga umehalalishwa nchini India

Soma pia: Canada yatangaza kusitisha ofisi za kibalozi India

Inaweza kuonekana kuwa hakuna mtu anayetaka kurudia hali iliyojitokeza kwa Canada, hasa wakati ambapo uhusiano kati ya New Delhi na Washington ukizidi kukua katika miaka ya hivi karibuni. Mnamo Juni, baada ya Nijjar kuuawa nchini Kanada lakini kabla ya Ottawa kuelezea mashaka yake juu ya kuhusika kwa India, Waziri Mkuu Narendra Modi alitembelea Marekani kutia saini mikataba kadhaa ya ulinzi, safari za anga na biashara. Rais wa Marekani Joe Biden aliitembelea India kwa ajili ya mkutano wa kilele wa G20 Septemba mwaka huu.

Mtaalamu wa sera ya kigeni C. Raja Mohan aliiambia DW kwamba haoni mtafaruku wowote mkubwa au mpasuko wa kidiplomasia ukitokea kati ya Washington na New Delhi.

"Tukio linalodaiwa lilitokea Juni. Kumekuwa na ushirikishwaji mkubwa juu ya suala hili kati ya taasisi mbili za usalama na uongozi wa kisiasa katika miezi michache iliyopita," alisema Mohan, ambaye ni profesa mgeni katika Taasisi ya Mafunzo ya Asia Kusini huko Singapore.

"Wakati mahakama ikichukua kesi hiyo, India imesema mauaji nje ya nchi sio sera yake na kwamba itachunguza suala hilo na kuwaadhibu watakaopatikana na hatia. Wakati huo huo, ziara za ngazi ya juu zinaendelea katika pande zote mbili na maandalizi yanaendelea kwa ajili ya mkutano wa Quad mjini Delhi mapema mwaka ujao ambao utahusisha ziara ya Rais Biden nchini India," aliongeza.

India | Mkutano wa G20| Narendra Modi na Joe Biden
Marekani na India zimeimarisha uhusiano wao kwa kiwango kikubwa.Picha: AFP

Balozi  wa zamani Anil Wadhwa pia anaamini athari ya madai ya njama ya mauaji itakuwa ndogo. "Ni vigumu kufikiria kuwa suala hili linaweza kuvuruga uhusiano imara wa pande zote ambao tayari umeendelezwa kati ya India na Marekani," aliiambia DW.

Kwanini Marekani inaihitaji India?

Utawala wa Biden unaiona India kama mshirika muhimu na katikati mwa changamoto za kijiografia kama vile vita vinavyoendelea vya Israel-Hamas na upanuzi wa kijeshi wa China katika eneo la Indo-Pacific.

Soma pia: India yamfukuza balozi wa Canada

Washington inaonekana hasa kutaka kuratibu masuala ya usalama. Mapema Agosti, mshauri wa usalama wa taifa Jake Sullivan alikutana na mwenzake, Ajit Doval, ana kwa ana wakati wa mkutano kuhusu mzozo wa Ukraine mjini Jeddah.

Hii ilifuatiwa na mkuu wa CIA William Burns kukutana na Ravi Sinha, mkuu wa wakala wa kijasusi wa nje wa India huko New Delhi.

Varun Sahni, profesa wa siasa za kimataifa katika Chuo Kikuu cha Delhi cha Jawaharlal Nehru, alisema uhusiano wa New Delhi na Washington uko katika ligi tofauti kabisa na uhusiano wake na Ottawa.

"Kwa sababu hiyo, athari katika mahusiano baina ya nchi hizo mbili na Marekani haziwezi kuakisi mporomokowa mahusiano na Canada," Sahni aliiambia DW.