1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Novemba 11: Miaka 100 ya kumalizika vita vikuu vya kwanza

Zainab Aziz
10 Novemba 2018

Miaka 100 iliyopita tarehe 11 mwezi Novemba mnamo mwaka 1918 mamilioni ya askari waliweka chini silaha zao. Hiyo ilikuwa siku ya kumalizika vita vikuu vya kwanza.

https://p.dw.com/p/381Qm
Kushoto: Kansela wa Ujerumani Angela Merkel. Kulia: Rais wa Ufaransa Emmanuel Macro
Kushoto: Kansela wa Ujerumani Angela Merkel. Kulia: Rais wa Ufaransa Emmanuel MacronPicha: Getty Images/AFP/A. Jocard

Ujerumani iliyokuwamo katika mapambano dhidi ya mataifa makubwa ilisambaratika kijeshi, kiuchumi na kisiasa. Na tangu wakati huo siku hii ya tarehe 11 mwezi wa 11 inakumbukwa, kila mwaka kama siku ya kumalizika vita vikuu vya kwanza. Kumbukumbu hiyo itafanyika katika eneo la Arc de Triomphe, Champs-Elysees mjini Paris.

Viongozi wa dunia ikiwa pamoja na kansela wa Ujerumani Angela Merkel, rais Donald Trump wa Marekani rais Vladimir Putin wa Urusi na waziri mkuu wa Uingereza Theresa May pamoja na mwenyeji wao rais wa Ufaransa Emmanuel Macron watahudhuria halfa ya kumbukumbu hiyo. 

Tarehe 11 mwezi Novemba mnamo mwaka 1918  mabalozi wa Ujerumani na kutoka mataifa yaliyofungamana, walikutana ndani ya  behewa la  treni na walitia saini hati ya kusimamisha mapigano yaliyosababisha vifo vya askari zaidi ya milioni 10 na raia milioni 6.

Mwenendo wa vita kwa manufaa ya nchi zilizofungamana, Ufaransa na Uingereza ulibadilika baada ya majeshi ya Marekani kuingia katika vita hivyo. Rais Donald Trump amesema kabla ya kuanza siku mbili za kumbukumbu ya vita hivyo kwamba nchi yake inabeba mzigo mkubwa sana katika ulinzi wa nchi za magharibi. Rais huyo pia alisema hapo awali kwamba pendekezo la rais Macron juu ya nchi za Umoja wa Ulaya kuunda jeshi lao ni kauli ya kukashifu.

Merkel na Macron waweka shada la maua kwenye eneo palipofikiwa makubaliano ya kumaliza vita vikuu vya kwanza
Merkel na Macron waweka shada la maua kwenye eneo palipofikiwa makubaliano ya kumaliza vita vikuu vya kwanza Picha: Getty Images/AFP/A. Jocard

Hata hivyo ofisi ya rais mjini Paris imesema kauli ya rais Macron imetafsiriwa vibaya na rais Trump. Viongozi hao wamekutana kwa ajili  ya mazungumzo baada ya tofauti baina yao kutokea. Pande zote mbili zimejaribu kuzisawazisha tofauti baina yao huku rais Trump  akiahidi  kwamba Marekani itazisaidia nchi za Ulaya  katika masuala  ya ulinzi lakini pia amezitaka nchi hizo ziubebe mzigo wa  gharama kwa njia ya usawa.

Wakati huo huo kansela wa Ujerumani Angela Merkel na mwenyeji wake rais wa Ufaransa Emmanuel Macron wameitembelea sehemu ambako hati ya kumaliza vita hivyo ilitiwa saini katika eneo hilo umbali wa  kilometa 56 kaskazini mashariki mwa mji wa Paris ambako Merkel na Macron watafanya tukio la ishara ya kutiliana saini.

Vikosi vya Ujerumani na Ufaransa vitafanya gwaride la pamoja kuwakumbuka wanajeshi milioni 1.4 wa Ufaransa na wanajeshi wa Ujerumani milioni 2 waliouawa katika vita hivyo. Takriban watu milioni 40 walikufa kwenye vita hivyo, miongoni mwao milioni 11 walikuwa ni wanajeshi.

mwandishi:Zainab Aziz/DPA

Mhariri: Lilian Mtono