1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Olaf Scholz aapa kufanya kazi na Israel kupeleka msaada Gaza

Amina Mjahid
19 Oktoba 2023

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amewaambia wabunge wa Ujerumani kwamba taifa hilo linasimama pamoja na Israel na kwamba msaada wa kibinaadamu, ni lazima uwafikie raia wa Palestina wanaopitia hali ngumu.

https://p.dw.com/p/4XkP8
Ujerumani | Bundestag Olaf Scholz
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz, alipokuwa akilihutubia bunge la Ujerumani Bundestag mjini Berlin.Picha: Annegret Hilse/REUTERS

Kansela huyo wa Ujerumani alilihutubia bunge la Ujerumani Bundestag baada ya ziara yake nchini Israel siku ya Jumanne. Scholz amesema katika wakati huu mgumu, Ujerumani ipo upande wa Israel, akiongeza kwamba raia wa Gaza ni lazima wapate msaada wa kiutu na utoaji wa msaada huo ni lazima pia, uwe sehemu ya mkakati wowote ule wa kusonga mbele. Amesisitiza kwamba Israel ina haki ya kujilinda.

Kansela huyo wa Ujerumani amesema tayari ameshazungumza na Israel, Jordan na Misri kutafuta njia ya kufikisha misaada mjini Gaza. Ameongeza kuwa katika mazungumzo yake na viongozi hao wa kikanda, alielezea umuhimu wa kudhibiti mapigano hayo ili kuzuwiya yasisambae katika eneo zima la Mashariki ya kati, kwamba juhudi zote zinapaswa kuchukuliwa kuepusha hilo kutokea.

Israel kuruhusu uingizwaji misaada ya kiutu Gaza kupitia Misri

Ametahadharisha kwamba itakuwa kosa kubwa kwa Iran au kundi la wanamgambo wa Hezbollah kuingilia vita hivyo vinavyoendelea kati ya Israel na Hamas. Kiongozi huyo wa Ujerumani amesema jambo muhimu lililobakia hivi sasa ni kuhakikisha watu waliochukuliwa mateka na kundi la Hamas, wanaachiwa huru bila masharti yoyote. Scholz amesema aliona nyuso zilizojaa hofu wakati alipozungumza na baadhi ya jamaa za watu hao alipokuwa ziarani mjiniTel Aviv siku ya Jumanne.

Scholz asema Ujerumani itapambana na chuki dhidi ya wayahudi 

Kanzler Scholz in Israel | Pk mit  Netanjahu
Kansela wa Ujeruman Olaf Scholz akiwa na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu mjini Tel Aviv, IsraelPicha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Kando na hayo Scholz amesema Baraza la Ulaya limeungana katika kuiunga mkono Israel na akasisitiza kwamba visa vya chuki dhidi ya Wayahudi havina nafasi Ujerumani, na taifa hilo halitaruhusu kamwe maandamano ambayo matamshi hayo yatatumika. Ameyasema hayo baada ya kisa cha hivi karibuni cha sinagogi la kiyahudi lililoko mjini Berlin kushambuliwa kwa mabomu. Shambulio hilo limetokea wakati visa vya chuki dhidi ya wayahudi vikiongezeka kufuatia mzozo unaoendelea kati ya Hamas na Israel.

Biden: Nimechukizwa na shambulio la hospitali Gaza

Mzozo  huo ulianza tarehe 7 baada ya kundi la Hamas kufanya mashambulizi kusini mwa Israel na kuwauwa takriban watu 1300. Palestina imeripoti mauaji ya zaidi ya watu 3,000 kufuatia na mzozo huo.  Marekani, na Umoja wa Ulaya ikiwemo Ujerumani, zinalitaja kundi la Hamas kuwa shirika la kigaidi.

Chanzo: Ukurasa wa Kingereza wa DW