1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Juhudi zaidi zahitajika kukabiliana na athari za mazingira

Babu Abdalla 2 Desemba 2019

Rais wa kamisheni ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen ameonya ulimwengu huenda ukalipa gharama kubwa zaidi iwapo viongozi watakosa kushughulikia ipasavyo suala la mabadiliko ya tabia nchi.

https://p.dw.com/p/3U6F9
Deutschland Europa-Rede Ursula von der Leyen
Picha: Reuters/A. Hilse

Suala la mabadiliko ya tabia nchi limekuwa kinywani mwa viongozi mbalimbali duniani hasa baada ya Greta Thunberg kuanzisha harakati za mabadiliko ya hali ya anga kwa kuwatolea wito viongozi duniani kuchukua hatua madhubuti kulishughulikia suala hilo.

Rais wa halmashauri ya Ulaya Ursula von der Leyen ameonya kuwa ulimwengu huenda ukalipia gharama kubwa zaidi iwapo viongozi watalifumbia macho suala la mabadiliko ya tabia nchi. Onyo hilo amelitoa ikiwa ni siku yake ya pili kuhudumu ofisini kama rais wa tume ya Ulaya.

Von der Leyen ameongeza kuwa tume hiyo inatarajiwa kuzindua mpango mpya wa kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabia nchi katika muda wa siku 10, unaojulikana kama mpango wa Ulaya ya Kijani.

Katika mpango huo, halmashauri ya Ulaya itatoa kima cha Euro trilioni moja kwa ajili ya uwekezaji endelevu na kuubadilisha umoja wa Ulaya katika muda wa muongo mmoja.

"Siku kumi kutoka sasa, halmashauri mpya ya umoja wa Ulaya utawasilisha mpango wa Ulaya ya kijani na iwapo lengo letu ni kuwa bara ambalo halitafika kiwango cha kupunguza gesi ya sumu ifikapo mwaka 2050 basi inabidi tuanze sasa kuzitekelza sera hizo kwa sababu ni mabadiliko ya kizazi," alisema Ursula von der Leyen amesema.

Guterres atoa wito kwa viongozi kuongeza juhudi za kukabiliana na athari za mazingira

Spanien Madrid Antonio Guterres vor der 25. UN-Klimakonferenz
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio GuterresPicha: picture-alliance/Europa Press/J. Hellin

Naye katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akihutubia kongamano hilo, pia amewatolea wito viongozi duniani kuongeza juhudi za kupambana na mabadiliko ya tabia nchi. Guterres amesema kuwa iwapo hali haitabadilika, basi usalama na afya ya viumbe vyote duniani iko hatarini.

Katibu mkuu huyo ametoa orodha ndefu ya ishara za wazi za kutia wasiwasi kuhusu athari ya mabadiliko ya tabia nchi ikiwemo takwimu mpya zilizotolewa na shirika la hali ya hewa duniani WMO.

Guterres amewatolea mwito pia viongozi wote wa kisiasa waliofika katika mkutano huo kuongoza kwa vitendo na wala sio kufuata tu. Na ni jukumu la viongozi wa siasa kuongoza katika kuhusika na kufaidika na harakati hizi  ili kupata ushindi dhidi ya suala la mabadiliko ya tabia nchi.

Kwa mujibu wa shirika la hali ya hewa duniani WMO, viwango vya joto vimepanda kwa kiasi cha kutisha katika muda wa miaka mitano iliyopita na pia mkusanyiko wa hewa ya mkaa angani umefikia kiwango ambacho hakijawahi kuonekana katika muda wa kati ya miaka milioni 3 hadi 5.

Chanzo dpa