1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Pakistan yatafakari kuendelea na uchaguzi Januari

31 Desemba 2007
https://p.dw.com/p/CiGs

ISLAMABAD

Maafisa wa uchaguzi nchini Pakistan wamekuwa na mkutano wa dharura hapo jana na wanatazamiwa kuendelea nao tena leo hii kuamuwa iwapo au la kuendelea na uchaguzi uliopangwa kufanyika hapo mwezi wa Januari katika taifa ambalo limetumbukizwa kwenye mgogoro kutokana na kuuwawa kwa kiongozi wa upinzani nchini humo Banazir Bhutto.

Chama cha Bhutto hapo jana kimemchaguwa mtoto wake wa kiume na mume wake kuchukuwa nafasi yake lakini wasi wasi umekuwa ukizidi kuongezeka iwapo uchaguzi huo wa bunge uliokusudia kuiondowa Pakistan katika utawala wa kijeshi na kuirudisha kwenye utawala wa kiraia utafanyika kama ilivoypangwa hapo tarehe nane mwezi wa Januari.

Mtoto wa kiume wa Bhutto mwenye umri wa miaka 19 aliyejulishwa kwenye mkutano wa waandishi wa habari kama Bilawal Bhutto Zardari amesema mapambano ya muda mrefu ya chama chake kuwania demokrasia yatalipiza kisasi cha mama yake.

Wakati huo huo Rais Pervez Musharraf wa Pakistan amekubali kufikiria msaada wa kimataifa kuchunguza mauaji ya waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo Benazir Bhutto.