1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Poland yaendelea na maombolezo ya wiki nzima

Josephat Nyiro Charo12 Aprili 2010

Poland leo imeanza kujaza nafasi za nyadhifa zilizoachwa wazi baada ya viongozi wakuu serikalini, akiwemo rais Lech Kaczynski, kuuwawa katika ajali ya ndege siku ya Jumamosi na kuliacha taifa hilo kuzama katika huzuni

https://p.dw.com/p/Muir
Watu wakiwasha mishumaa mbele ya ikulu ya rais mjini WarsawPicha: AP

Kufikia sasa ni miili 17 tu kati 96 ambayo imepatikana kutoka kwa vifusi vya ndege hiyo iliyoanguka Smolensk, Urusi.

Wachunguzi wa Urusi waliweza kuutambua mwili wa Bi Maria aliyekuwa mkewe rais Kaczynski wa Poland kutoka katika vifusi vya ndege ya Urusi iliyoanguka siku ya jumamosi.

Wachunguzi wanaofuatilia matukio ya janga hilo wamesema ndege hiyo iliingia katika ukungu kabla ya kugonga miti karibu na uwanja wa ndege wa Smolensk siku ya jumamosi. Kuna madai kwamba rubani wa ndege hiyo alipuuza maelezo ya waelekezi wa ndege ya kutotua.

Vyombo vingine vya habari nchini Poland vinadai kwamba huenda marehemu rais Kaczynski alitoa amri ya rubani atue ingawa mwendesha mashtaka wa Poland, Andrzej Seremet amesema kwa sasa hakuna ushahidi kudhibitisha hoja hiyo.

Kifo cha makamanda wa kijeshi, viongozi wa ngazi ya juu wa upinzani na gavana wa benki kuu ya Poland kimeacha pengo kubwa kwa uongozi wa nchi hiyo yenye idadi ya raia milioni 38 na ilioo ndani ya Umoja ya Ulaya na ni mwanachama wa Jumuiya ya Kujihami ya magharibi ya NATO.

Kaimu wa rais, Bronislaw Komorowski, aliyepangiwa kuchuana vikali katika uchaguzi wa mwezi Oktoba, amesema leo kwamba amejaza nafasi za nyadhifa zilizoachwa wazi katika uongozi wa juu wa nchi hiyo.

Komorowski alisema katika marekebisho, atakalolipa kipau mbele ni kufanyiwa marekebisho sheria ya usafiri wa viongozi wa kijeshi.

Kaimu huyo wa rais pia alisema atatenga tarehe ya uchaguzi war ais baada ya kufanya mazungumzo na viongozi wa vyama vya kisiasa nchini Poland.

Jeneza la marehemu Kaczynski litawekwa nje ya ikulu ili kuwapa nafasi raia wa Poland kutoa heshima zao za mwisho kuanzia kesho.

Mwendesha mashtaka nchini Poland amedhibitisha kwamba bado kuna miili iliyokwama ndani ya vifusi vya ndege iliyohusika katika ajali hiyo.

Mwandishi, Peter Moss/Reuters/AFP

Mhariri, Othman Miraji