Polisi wapambana na wafuasi wa upinzani Iran
7 Desemba 2009Kwa mujibu wa ripoti za mashahidi,polisi walifyetua risasi na walitumia gesi ya kutoa machozi, kuwatawanya waandamanaji wa upinzani. Mapambano hayo yalitokea katika vyuo vikuu kadhaa na katika mitaa maarufu ya mji mkuu Tehran uliojaa vikosi vya polisi wa kuzuia ghasia. Gesi ya kutoa machozi ilitumiwa dhidi ya wafuasi wa kiongozi wa upinzani Mirhossein Mousavi baada ya ghasia kuzuka kati kati ya Tehran wakati wa mkutano rasmi wa kuadhimisha kukumbukumbu ya wanafunzi watatu waliouawa na polisi wakati wa utawala wa Shah, kiongozi wa zamani wa Iran.
Mkutano huo ulifanywa katika chuo kikuu cha Tehran ili kuwazuia waandamanaji wa upinzani. Shahidi mmoja amesema kama polisi 1,000 walikizingira chuo kikuu hicho na askari kanzu walikuwa wakipiga picha yale yaliyokuwa yakitokea ndani ya uwanja wake. Vile vile amesema kuwa kama watu 10 walikamatwa.
Kwa mujibu wa tovuti ya wapenda mageuzi Rah-e Sabz miongoni mwa wale waliokamatwa ni wafuasi wawili wa kike wa kiongozi wa upinzani Moussavi. Lakini habari hizo hazikuweza kuthibitishwa na vyombo huru vya habari kwa sababu waandishi wa habari wa kigeni, hawana ruhusa ya kutoka nje ya ofisi zao na kuripoti yale yanayotokea kuanzia tarehe 7 hadi 9 Desemba.
Serikali vile vile imeufunga mtandao wa simu za mkono mjini Tehran ili kuzuia mawasiliano kati ya waandamanaji wa upinzani. Hatua za usalama zilizochukuliwa na serikali wakati wa maadhimisho ya "Siku ya Wanafunzi" zimedhihirisha jinsi viongozi hao walivyoazimia kuuzima upinzani nchini humo. Hata hivyo, siku ya Jumapili Muossavi alisema kuwa shughuli zao za upinzani zitaendelea licha ya shinikizo la serikali. Yeye amewahimiza wafuasi wake kuandamana barabarani kupinga ukandamizaji wa wanafunzi.
Wanamgambo wa kujitolea-maarufu kama Basij- walio washirika wa Walinzi wa Mapinduzi ya Iran ambao ni ngome ya serikali ya Ahmedinejad, waliwaonya wapinzani kutoutumia mkutano wa leo kuchochea upya maandamano dhidi ya serikali. Makundi hayo mawili yalizima maandamano ya upinzani kufuatia uchaguzi wa mwezi wa Juni na maelfu ya watu waliwekwa mbaroni.
Wengi wao wameachiliwa huru lakini hadi sasa zaidi ya watu 80 wamefungwa kwa hadi miaka 15 na wengine 5 wameadhibiwa kifo. Wapinzani wa serikali wanaogombea mageuzi wanasema kuwa zaidi ya watu 70 waliuawa katika machafuko yaliyozuka baada ya uchaguzi wa Juni. Lakini serikali inakanusha na kusema kuwa idadi ya waliouawa ni nusu ya hao wakiwemo pia wanamgambo wa Basij.
Mwandishi: P.Martin/AFPE/RTRE
Mhariri: M.Abdul-Rahman