1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Kenyatta na Odinga wazindua zoezi la kukusanya sahihi

Shisia Wasilwa25 Novemba 2020

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na Kiongozi wa Chama cha ODM Raila Odinga wamezindua zoezi la ukusanyaji wa sahihi kwa lengo la kuunga mkono ripoti ya Maridhiano ya taifa-BBI.

https://p.dw.com/p/3lou9
Kenia Präsident Uhuru Kenyatta und Oppositionsführer Raila Odinga in Nairobi
Picha: Reuters/T. Mukoya

Rais Kenyatta amewaambia Wakenya kuwa BBIni njia ya kuleta umoja katika taifa na kuwataka wanasiasa kukoma kupiga siasa za mgawanyiko. 

Kimsingi hatua ya kuzindua ripoti hiyo leo, inafunga mlango wa kufanyiwa marekebisho ripoti yenyewe na kuanzisha safari ya kufanyiwa marekebisho katiba iliyoidhinishwa mwaka 2010.

Soma pia: Wabunge wa Kenya wagawika kuhusu utekelezaji wa ripoti ya BBI

Sekretariati ya BBI inayoongozwa na mbunge wa Suna Mashariki na mbunge wa zamani wa Dagorreti Kusini, Dennis Waweru wamesema kuwa wanatarajia kupata sahihi milioni moja katika kipindi cha siku saba zijazo.

Naibu wa rais William Ruto ambaye amekuwa akishinikiza ripoti ya BBI ifanyiwe marekebisho hakuhudhuria hafla ya kuzindua zoezi la kukusanya sahihi.
Naibu wa rais William Ruto ambaye amekuwa akishinikiza ripoti ya BBI ifanyiwe marekebisho hakuhudhuria hafla ya kuzindua zoezi la kukusanya sahihi.Picha: picture-alliance/Photoshot/P. Siwei

Uzinduzi wa ripoti yenyewe uliahirishwa juma lililopita baada ya rais Kenyatta kufanya kikao na makamu wake William Ruto kwa kile kilichoripotiwa ni kutafuta uwiano.

Hata hivyo, hatua ya leo inamuacha makamu wa rais katika njia panda, ya kuunga mchakato wenyewe ama kuupinga. Ruto hakuhudhuria hafla za leo. Akiizindua ripoti yenyewe rais Uhuru Kenyatta amewataka Wakenya kuikubali ripoti hiyo kwa manufaa yao.

Baada ya mswada wenyewe kuchapishwa, Wakenya watakuwa na nafasi ya kupata nakala ambazo zitasambazwa kila pembe ya nchi.

Katiba ya sasa ya KEnya iliidhinishwa mwaka 2010 chini ya utawala wa rais wa zamani MWai Kibaki
Katiba ya sasa ya KEnya iliidhinishwa mwaka 2010 chini ya utawala wa rais wa zamani MWai KibakiPicha: Getty Images/AFP/T. Karumba

Maafisa serikalini kuchukua usukani kufanikisha zoezi hilo

Machifu watachukua usukani katika maeneo ya mashinani wakiongozwa na maafisa wakuu katika serikali kuu. Waasisi wa BBI wanasema kuwa kuhusishwa kwa maafisa wakuu serikalini kunalenga kufutilia mbali maslahi ya wanasiasa.

Mchakato wa marekebisho ya katiba ulioongozwa na Kiongozi wa ODM Raila Odinga ulifeli mwaka 2015 baada ya Tume Huru ya Kusimamaia Uchaguzi kushindwa kuthibitisha sahihi za wananchi. Ili kuepuka makosa kama hayo, waratibu watateuliwa katika kila jimbo na eneo bunge.

Raila Odinga ambaye ameonekana kukataa kufanyiwa marekebisho ripoti hiyo alichukua muda wake kuwakosoa wapinzani wa BBI.

Tume ya uchaguzi IEBC yaidhinisha ukusanyaji sahihi

Kufuati ombi la sekretariati, Tume Huru ya Kusimamia Uchaguzi na Mipaka-IEBC, iliidhinisha utaratibu utakaotumika kukusanya sahihi.

Wafula Chebukati, mwenyekiti wa tume inayosimamia uchaguzi Kenya IEBC
Wafula Chebukati, mwenyekiti wa tume inayosimamia uchaguzi Kenya IEBCPicha: picture-alliance/AP Photo/S. Abdul Azim

Watu watakaokubali kutia sahihi watahitajika kuandika majina yao, nambari ya kitambulisho, kaunti, eneo bunge, wadi, kituo cha kupigia kura, nambari ya simu na barua pepe. Alama za vidole zitawekwa kwenye fomu na kuthibitishwa na IEBC. Wakenya wamegawanyika kuhusu maoni yao.

Baadhi ya masuala tata ambayo yamekosolewa na viongozi wa dini na makamu wa rais William Ruto ni pamoja na kuundwa kwa Baraza la idara ya polisi, bodi huru ya kusimamia idara ya mahakama pamoja na mamlaka makubwa atakayokuwa nayo rais.

Baada ya sahihi kukusanywa, bunge litajidili mswada huo na ukisha kuudhinisha utapelekwa kwenye kura ya maoni.