1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Magufuli azindua mradi wa umeme wa mto Rufiji

Sylvia Mwehozi
26 Julai 2019

Rais John Magufuli ameuzindua mradi mkubwa wa uzalishaji umeme katika Mto Rufiji licha ya upinzani mkubwa kutoka kwa mataifa ya kigeni na asasi za mazingira zinazoukosoa mradi huo kutokana na uharibifu wa mazingira. 

https://p.dw.com/p/3Mmbn
Tanzania Hydro Power Projekt Stigler Gorge
Picha: DW/S. Khamis

Mradi huo ambao unajengwa kwa fedha za ndani upo katika eneo la Selous linalotajwa kuwa moja ya maeneo ya turathi za dunia, ambapo Tanzania inakusudia kupata umeme wa kutosha kupitia mradi huo. Ingawa mataifa ya kigeni yalionya kuhusu uharibifu wa mazingira katika eneo hilo, Rais Magufuli amesema Tanzania ni taifa huru lenye uwezo wa kujiamulia mambo yake hata kama mambo hayo yatawachukiza wengine:

"Natambua kuwa pamekuwepo na maneno, kuwa mradi huu utaharibu mazingira lakini kiukweli mradi huu unayajenga mazingira. Upinzani huo ulianza mara tu tulipotangaza kuanza kutekeleza mradi huu mwezi Juni 2017. Hata hivyo kwa kuwa nchi yetu ni huru na sio maskini, narudia nchi yetu huru na wala siyo maskini kama baadhi ya watu wanavyodhani. Tuliamua ni lazima tuutekeleze mradi huu, sisi hakuna mtu wa kutufundisha katika suala hili Tanzania. Tanzania ni kinara katika kuhifadhi mazingira", alisema rais Magufuli wakati akizindua mradi huo. 

Tanzania Hydro Power Projekt Stigler Gorge
Rais Magufuli akipewa maelezo kuhusu mradi wa kuzalisha umeme wa mto RufijiPicha: DW/S. Khamis

Mradi huo ambao unafahamika pia kwa jina la Stieglers Gorge, unatazamiwa kuzalisha megawati 2,000 za umeme, hatua ambayo inaelezwa kwamba itasaidia kupunguza tatizo la nishati hiyo muhimu kiuchumi na kijamii.

Hatua ya kuanza kwa mradi huo inakuja baada ya miaka 40 tangu utafiti wa uzalishaji wa umeme kutoka Mto Rufiji uliofanywa wakati wa utawala wa rais wa kwanza, Mwalimu Julius Nyerere. Ujenzi wa bwawa hilo unaofanywa na wakandarasi kutoka nchini Misri unatarajiwa kugharimu dola za Marekani bilioni 2.9 sawa na shilingi trilioni 6.5 za Kitanzania.

Rais Magufuli amesema walitumia muda kutafakari kuhusu mradi huu kwa sababu Tanzania imebarikiwa na vyanzo vingi vya uzalishaji umeme kama vile maji, gesi asilia, upepo, joto na makaa ya mawe.

Tanzania Hydro Power Projekt Stigler Gorge
Rais Magufuli aliambatana na viongozi wengine wa serikali Picha: DW/E. Boniphac

Wanaharakati na mashirika ya mazingira ndani na nje ya Tanzania wanasema kuwa ujenzi wa mradi huu unaweza kuleta madhara makubwa kwa viumbe hai pamoja na binaadamu wanaoishi katika eneo hilo.

Wachunguzi wa mambo wanasema kukamilika kwa mradi huo kutakuwa ni habari njema kwa sekta nyingi, ikiwemo ya viwanda ambayo wawekezaji wake wamekuwa wakilalamikia gharama kubwa za bei ya nishati ya umeme.

Hata hivyo, bado ni mapema kujuwa kipi kitayasibu mazingira baada ya mraddi huo unaotarajiwa kukamilika Juni 2022 kuanzan kazi rasmi.

Mwandishi: George Njogopa, Dar es Salaam