1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Ufaransa Sarkozy aizuru Chad

Abdulrahman, Mohamed27 Februari 2008

Jumuiya zinazopigania haki za binaadamu zimeitaka Ufaransa kutoficha ukweli kuhusiana na Rais Idriss Derby Itno ambaye ana

https://p.dw.com/p/DE9j
Rais Nicolas Sarkozy akifafanua jambo.Picha: AP

Rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa anaitembelea Chad akiwa njiani kuelekea Afrika kusini , huku jumuiya zinazopigania haki za binaadamu zikitaka Ufaransa kutoficha ukweli kuhusiana na Rais Idriss Derby Itno ambaye anashukiwa kuwa na mkono wake katika kutoweka kwa baadhi ya wanachama wa upinzani. Ziara ya Sarkozy inakuja wiki chache baada ya waasi kufika mji mkuu Ndjamena kujaribu kumuangusha Rais Derby, na kudai kwamba jaribio majeshi ya Ufaransa yalimsaidia kiongozi huyo kuzima uasi huo.

Kwa hakika Rais Sarkozy atakuweko Chad kwa muda mfupi tu, akiwa njiani kuelekea Afrika kusini. Wakati haiba yake nyumbani imeshuka , Sarkozy anafanya ziara hiyo akiwa na mkewe mpya Carla Bruni ambaye ziara hii kwake ni ya kwanza akiwa mke wa rais.

Sarkozy anatarajiwa kushinikiza juu ya kuundwa tume itakayochunguza kutoweka kwa wanachama wa upinzani Ngarlejy Yorongar na Ibni Oumar Mahamat Saleh.

Akiwa Chad atakula chakula cha usiku na wanajeshi wa Ufaransa ambao mapema mwezi huu wanasemekana waliyasaidia majeshi ya serikali kuwarudisha nyuma waasi walioingia hadi mji mkuu Ndjamena katika kiu chao cha kutaka kum´ngoa madarakani rais Derby.

Aidha ziara hiyo inafanyika katika wakati ambao Ufaransa inaliongoza jeshi la umoja wa ulaya EUFOR lililotumwa Chad kuwalinda wakimbizi walioko huko kutoka jimbo la magharibi mwa Sudan la darfur. Utulivu nchini Chad ni muhimu kwa mafanikio ya ujumbe huo wa umoja wa ulaya baada ya kuahirishwa kwa mufda hapo kabla kutumwa wanajeshi hao

Waziri wa Ufaransa anayehusika na ushirikiano Jean-Marie Bockel alisema Sarkozy atatoa shinikizo zito kwa Rais Derby kumtaka azilitumie hujuma ya waasi kama sababu ya kuwaandama wapinzani na kumtaka pia aharakishe mkondo wa demokrasia nchini humo.

Wakati huo huo Jumuiya ya kimataifa ya haki za binaadamu Amnesty International nimeitaka Uafaransa kumshinikiza rais Derby afafanue juu ya kutoweka kwa wabunge wawili wa upinzani tangu tarehe 3 mwezi huu.Akizungumza kutoka Newyork jana , waziri wa mambo ya nchi za nje wa Chad Ahmad Allam-Mi alisema mmoja wa wabunge hao Bw Yarongar yuko Ndjamena na huenda maelezo juu ya kukamatwa kwake yakatolewa leo. lakini haikuweza kufahamika hatima ya Bw Saleh. Mashirika ya haki za binaadamu yamekua na wasi huenda wakateswa wakiwa kizuizini.

Rais Sarkozy ataelekea baadae Afrika kusini hapo kesho na ziara yake hiyo hadi Ijumaa inatarajiwa kutuwama katika ushirikiano katika sekta ya nishati, huku kampuni kubawa ya nuklea ya Ufaransa AREVA inawania kupata kandarasi ya ujenzi wa vinu vya nuklea dhidi ya kampuni moja ya umeme ya Marekani.

Sarkozy atalihutubia bunge mjini Cape town, hotuba ambayo itafuatiliwa kwa makini baada ya hotuba aliyoitoa mjini Dakar Senegal mwezi Julai ambayo ililaaniwa ikitajwa kuwa ilikua ya ubaguzi. Katika hotuba hiyo Sarkozy aliseama waafrika hawana budi kugeukia maendeleo na kwamba ukoloni haupaswi kulaumiwa kwa maovu yote ya bara hilo.

Siku ya Ijumaa rais huyo wa Ufaransa atakutana faragha na shujaa wa Afrika kusiniwa mapambano dhidi ya sera ya ubaguzi Mzee Nelson Mandela mwenye umri wa miaka 89. Ziara ya Sarkozy nchini Afrika kusini inathihirisha nia ya Ufaransa yakuendeleza ushirikiano na taifa hilo kubwa la kiuchumi barani Afrika.