1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Shinikizo linazidi dhidi ya watawala wa kijeshi Myanmar

Mohammed Abdul-Rahman28 Septemba 2007

Mataifa kadhaa katika baraza la haki za binaadamu la Umoja wa mataifa yameanza mashauriano njuu ya uwezekano wa kuitishwa kikao maalum kuitathimini hatua za matumizi ya nguvu za utawala wa kijeshi nchini Myanmar. Kukandamiza maadamano ya amani ya wiki hii katika miji kadhaa nchini humo. Maandamano hayo yamekua yakiongozwa na watawa wa dini ya Budha kudai demokrasia na kuungwa mkono na raia. Wakati huo huo umoja wa mataifa umemtuma mjumbe wake maalum kwenda Yangon kuzungumza na watawala wa kijeshi.

https://p.dw.com/p/CB0t
Kiongozi mpigania demokrasia Aung Suu-Kyi ambaye kwa miaka kadhaa amewekwa katika kizuizi cha nyumbani na wanajeshi.
Kiongozi mpigania demokrasia Aung Suu-Kyi ambaye kwa miaka kadhaa amewekwa katika kizuizi cha nyumbani na wanajeshi.Picha: AP

Ujumbe wa Uingereza umekua katika pirika pirika za kuwarai wanachama wengine 47 katika baraza hilo la haki za binaadamu la umoja wa mataifa, kutafuta uungaji mkono kwa ajili ya kikao maalum . Kulingana na sheria za baraza hilo, ombi la aina hiyo halina budi liungwe mkono na wajumbe 16 ili iliweze kujadiliwa.

Wajumbe waliohutubia baraza hilo jana walielezea wasi wasi wao kuhusiana na hatua kali zilizochukuliwa na wanajeshi dhidi ya waandamanaji wiki hii na kuwataka watawala wa Burma wanaoiita nchi hiyo Myanmar kuwa na subira katika kukabiliana na maandamano hayo, na kuwakumbusha wajibu wao kwa mujibu wa sheria za kimataifa la kulinda usalama wa raia wote wanaoandamana kwa amani.

Taarifa kutoka mji mkuu wa Myanmar- Yangon zinasema kiasi ya watu 14 waliuwawa katika maandamano ya Jumatano na jana Alhamisi, wengi kadhaa kujeruhiwa na mamia kutiwa nguvuni.

Kabla ya kikao cha sita cha wiki tatu cha baraza hilo kumalizika leo, panapaswa kufikiwa uamuzi juu ya uwezekano wa kuitishwa mjadala maalum kuhusu hali ya mambo nchini Myanmar.

Hadi sasa nchi za Asia na hasa zile zilizo karibu sana ana Burma zimeonyesha hali ya shaka shaka na kuna fununu miongoni mwa duru za kibalozi kwamba zitalipinga wazo hilo. Jumuiya za kiraia hata hivyo zinaliunga mkono vilivyo wazo hilo.

Mjini Newyork katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki-moon amemtuma mjumbe wake maalum kwenda Myanmar kutathimini hali ya mambo ilivyo. Watawala wa kijeshi wanasemekana wamekubali kukutana na mjumbe huyo Ibrahim Gambari kutoka Nigeria. Marekani kwa upande wake imedai Bw Gambari aruhusiwe kukutana na pande zote zinazohusika wakiwemo wafungwa wa kisiasa na kiongozi anayepigania demokrasia Bibi Aung Suu Kyi ambaye kwa miaka sasa amewekwa katika kizuizi cha nyumbani.

Wakati huo huo Inaelekea Majenerali nchini Myanmar sasa wameyakata mawasiliano yote ya Internet kuzuwia utumaji zaidi nje ya nchi wa picha za video na barua pepe kuhusu yanayotokea nchini humo na upinzani mkubwa dhidi ya utawala huo wa kijeshi kuwahi kuonekana katika kipindi cha karibu miaka 20.

Kwa upande mwengine waziri mkuu Soe Win anayesadikiwa kuwa na umri wa miaka 58 anaendelea kubakia katika hospitali moja nchini Singapore alikolazwa kwa matibabu tangu miezi mitatu-minne iliopita. Win anashukiwa kuwa ndiye aliyekua nyuma ya hatua za kupambana na wanaharakati wa upinzani nchini Myanmar miaka minne iliopita .Lakini tangu wakati huo jitihada za waandishi habari kujaribu kujua hospitali aliko hazijafanikiwa.