1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Solskjaer awataka wachezaji wake kujiimarisha

16 Septemba 2021

Meneja wa Manchester United Ole Gunnar Solskjaer amemtolea mwito mchezaji wake Jesse Lingard kuimarisha mchezo wake kufuatia kosa alilolifanya katika mchuano wa ligi ya mabingwa Champions League dhidi ya Young Boys.

https://p.dw.com/p/40OLf
Europa League Finale | Villarreal v Manchester United
Picha: Kacper Pempel/REUTERS

Licha ya kosa hilo, Solskjaer amemuondolea lawawa Lingard kwa kusema "Hakuna mchezaji anayependa kufanya makosa, lakini ndio hali ya kandanda.Tutajifunza kutokana na kosa hilo, Lingard pia bila shaka atajifunza. Sisi sote ni binadamu, na kila mwanasoka hufanya makosa."

Manchester United nusra itoke sare ya 1-1 na Young Boys nchini Uswizi lakini kosa la dakila za mwisho la Lingard, lilimuwezesha Jordan Siebatcheu wa Young Boys kufunga bao la pili na la ushindi uwanjani Stadion Wankdorf mjini Bern.

Soma zaidi: Rashford alalamikia ubaguzi wa rangi

Manchester United ilitangulia kufunga bao kupitia kwa mchezaji wao nyota Cristiano Ronaldo kunako dakika ya 13 ya mchezo kabla ya Young Boys kusawazisha dakika ya 66 kupitia Nicolas Ngamaleu kabla ya Siebatcheu kufunga bao la ushindi.

Beki wa Manchester United Aaron Wan-Bissaka alipewa kadi nyekundu baada ya kucheza vibaya.

Timu hiyo inayotiwa makali na Ole Gunnar Solskjaer itaingia tena uwanjani mnamo siku ya Jumapili, Septemba 19 kucheza na West Ham United katika pambano la ligi kuu ya Premia.

Manchester United inaongoza jedwali la ligi ya Premia wakiwa na alama 10, wakati Westham United iko katika nafasi ya nane wakiwa na alama nane.