1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Steinmeier anaanza ziara Cuba

Admin.WagnerD16 Julai 2015

Steinmeir atakuwa waziri wa kwanza wa mambo ya nje wa Ujerumani kufanya ziara nchini humo tangu kuungana tena kwa Ujerumani miaka 25 iliyopita Sudi Mnette anaarifu zaidi

https://p.dw.com/p/1FzuN
Steinmeier außenminister wien
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Frank-Walter SteinmeierPicha: picture-alliance/dpa/EPA/H. Punz

Malengo ya ziara ya Steinmeier yanajikitia katika kustawisha uhusiano baina ya serikali za mataifa hayo mawili, yaani Ujerumani na Cuba. "Cuba na maeneo mengine ya ulimwengu wanajongeleana pamoja baada ya kipindi kirefu cha hali ya kutoaminiana". Alisema Steinmeier, na kuongeza kuwa ziara yake ina lengo la kufungua milango zaidi kati ya Cuba na maeneo mengine ya ulimwengu.

Historia ya uhusiano

Historia inaonesha maafisa wa ngazi ya juu kutoka kwa upande wa iliyokuwa Ujerumani Mashariki walitembelea Cuba, kwa wakati huo, lakini hakuna waziri yeyote kutoka kwa iliyokuwa Ujerumani Magharibi aliyefanya safari kama hiyo baada ya mapinduzi ya kikomunisti ya 1959.

Kuba Präsident Raul Castro im Parlament
Kiongozi Cuba Raul CastroPicha: Imago/Xinhua

Waziri wa mwisho kutembelea Cuba alikuwa, waziri wa zamani wa Uchumi Werner Mueller mwaka 2001. Hata hivyo hakuna waziri yeyote wa mambo ya nje aliyefanya ziara ya kutembelea Cuba tangu muungano wa Ujerumani mwaka 1990.

Kwa mujibu wa ratiba ya ziara ya Steinmeier nchini Cuba, waziri huyo anapaswa kufanya mazungumzo leo hii na kesho na mawaziri kadhaa wa taifa hilo, askofu mkuu wa Havana, Kadinali Jaime

Lucas Ortega Alamin, sambamba na wadau wengine wanaofanya kazi katika sekta ya utamaduni na asasi za kiraia.

Ziara hii inafanyika siku chache baada ya Cuba na Marekani kufungua upya balozi zake katika mataifa hayo, kufuatia jitihada za rais Barack Obama za mwaka jana za kuondosha tofauti iliyodumu kwa miongo mitano baina ya mataifa hayo mawili, kwa kuamrisha kuwepo kwa jitihada kamili za kidiplomasia kati ya serikali za Havana na Washington.

Cuba kwa upande wake imechukua hatua katika miaka ya hivi karibuni kwa kuacha fursa ya uchumi huria kwa kuzijengea uwezo hatua za ujasiriamali na kufanya mabadiliko katika sekta ya kilimo. Hakuna mpango wa waziri Steinmeier kukutana na kiongozi wa mapinduzi ya Cuba Fidel Castiro, wala ndugu yake Raul Castro, ambaye kwa hivi sasa ndiye kiongozi wa taifa hilo.

Mwezi Aprili, Rais Obama alikutana na Raul Castro, ikiwa ni mara ya kwanza viongozi wa juu ya mataifa hayo, Marekani na Cuba kukutana na kuwa na mazunguzo madhubuti katika kipindi cha zaidi ya miongo mitano.

Katika ziara yake hii ya siku mbili waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Steinmeier ameambatana na wawakilishi wa wafanyabiashara wa Ujerumani. Biashara kati ya mataifa hayo mawili bado ya kiwango cha chini sana. Katika nafasi ya kusafirisha bidhaa nje ya Ujerumani Cuba, inashika nafasi ya 101 na katika nafasi ambayo Ujeruamani inaingiza bidhaa Cuba inashika nafasi ya 125.

Mwandishi: Sudi Mnette/DPAE
Mhariri:Josephat Charo