1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan: Ujerumani yatoa wito pande zote zijizuie

Zainab Aziz
14 Aprili 2019

Ujerumani imesema ina matumaini ya kufanyika uchaguzi huru nchini Sudan na imeuwasilisha mgogoro wa nchi hiyo kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na imesisitiza Omar al-Bashir afikishwe kwenye mahakama ya ICC.

https://p.dw.com/p/3GjwX
Sudan Demonstration in Khartum
Picha: picture-alliance/AP Photo

Katika mkutano na waandishi wa habari, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ujerumani Christopher Burger aliweka tahadhari wakati alipoisoma taarifa rasmi juu ya hali inayobadilika kwa haraka na isiyotabirika ya nchini Sudan.

Msemaji huyo alisema jambo la uhakika ni kwamba mnamo Aprili 11, jeshi katika jiji la Khartoum lilichukua udhibiti wa kituo cha televisheni cha taifa na kutangaza litatoa tamko baadaye juu ya hali ya kisiasa ya Sudan na na kwamba Rais wa muda mrefu Omar al-Bashir ameondolewa madrakani.

Hata hivyo, watu wengi waliiingia mabarabarani huko siku ya Ijumaa usiku ili kuendelea kuonyesha kwamba wanataka jamii huru, demokrasia nan chi itayoongozwa na serikali ya kiraia.

Msemaji huyo wa Wizara ya Mambo ya Nje Christopher Burger alitoa wito kwa pande zote zijizuie kwa sababu ufumbuzi wa amani katika mgogoro huo unahitajika na pia utakaozingatia matarajio ya watu wa Sudan wanaotaka mabadiliko.

Bwana Burger amesema Ujerumani, ambayo mwezi huu inashikilia urais wa zamu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, imeupa kipaumbele mgogoro wa Sudan kati ya ya ajenda zitakazo jadiliwa kwenye Umoja wa Mataifa pamoja na washirika wake wa Ulaya na Marekani.

Mnamo siku ya Alhamisi, Wizara ya Mambo ya Nje ilitoa tahadhari juu ya hali katika nchi hiyo ya Mashariki mwa Afrika na iliandikwa kwenye tovuti yake kwamba Usafiri wote usio muhimu kwenda nchini Sudan unapaswa kuepukwa, na viwanja vya ndege na mipaka kwa sasa imefungwa. Maandamano yanaweza kuendelea na kunauwezekano wa kuzuka vurugu zaidi hasa katika mji mkuu wa Khartoum.

Raia wa Sudan waandamana kusaka demokrasia katika mji mkuu wa Khartoum
Raia wa Sudan waandamana kusaka demokrasia katika mji mkuu wa KhartoumPicha: Getty Images/AFP/A. Shazly

Haijulikani bado alipo al Bashir lakini msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ameeleza kuwa msimamo wa Ujerumani upo wazi kwamba hati ya kukamatwa kwa al-Bashir iliyotolewa na ICC kwa madai ya uhalifu dhidi ya binadamu, uhalifu wa kivita na mauaji ya kimbari katika jimbo la Darfur bado ina nguvu.

Bashir mwenye umri wa miaka 75 anatumiwa kwa kuwatumia askari na jeshi lake kuyasakama kikatili makundi ya wachache huko Darfur Magharibi mwa Sudan mnamo mwaka 2003. Inakadiriwa watu 300,000 walipuawa katika vita hivyo. Uongozi mpya wa kijeshi wa nchini Sudan umesema al-Bashir atafunguliwa mashtaka nchini nan siyo nje ya Sudan.

Wanasiasa wa Ujerumani pia wanaunga mkono wito wa Wizara ya Mambo ya Nje kwamba al-Bashir afikishwe mbele ya mahakama ya mjini The Hague.

Gabi Weber, msemaji wa sera ya maendeleo kwa chama cha SPD katika bunge la Ujerumani hata hivyo ametoa wito kwamba kila kitu lazima kifanyike ili kuzuia tishio la kuzuka vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan.

Weber aliiambia DW kuwa hii inatokana na makundi mengi yaliyopo yana maslahi yasiyolingana ambayo yanapaswa kuwa na uwiano kwa kuzingatia amani ili mabadiliko ya kisiasa yaweze kufanikiwa. Amesema jumuiya ya kimataifa na serikali mpya ya Sudan wana jukumu la kuendelea kutoa msaada wa kibinadamu kwa wakimbizi milioni 3.5 wa Sudan.

Hata hivyo, muungano wa mashirika unaoendesha maandamano dhidi ya serikali ya Sudan, umetangaza kuwa hauamini matamshi ya uongozi wa kijeshi kuwa mamlaka yatakabidhiwakwa serikali ya kiraia.

Chanzo: //p.dw.com/p/3Gjtn