1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TEHRAN: Askari 15 wa Uingereza wachiliwa kwa msamaha wa rais

5 Aprili 2007
https://p.dw.com/p/CCCV

Iran imewaachilia huru askari 15 wa kikosi cha wanamaji cha Uingereza waliokamatwa wiki mbili zilizopita. Rais Mahmoud Ahmednejad aliitumia fursa wakati alipokuwa akihutubia kutangaza kuwa amewasamehe wanamaji hao wa Uingereza katika kile alichokitaja kuwa ni zawadi kwa raia wa Uingereza.

Baadae televisheni ya taifa ya Iran ilimuonyesha rais Ahmednejad akizungumza na wanamaji hao katika kasri yake mjini Tehran. Maafisa wa Iran wamefahamisha kuwa wanamaji hao watakabidhiwa kwa ubalozi wa Uingereza mjini Tehran leo hii.

Wanamaji hao watasafiri kwa ndege muda mfupi baadae.

Tehran imeeleza kuwa iliwakamata wanamaji hao wa Uingereza kwa kuingia ndani ya mipaka ya bahari ya Shatt al Arab nchini Iran bila idhini, ijapokuwa Uingereza inashikilia msimamo wake kuwa askari wake walikamatwa ndani ya bahari ya Irak.

Waziri mkuu wa Uingereza Tony Blair ameikaribisha hatua ya kuachiliwa askari hao 15 na kuushukuru umoja wa mataifa na nchi washirika wa Uingereza kwa juhudi zilizopelekea kuachiliwa askari hao wa Uingereza. Umoja wa Ulaya pia umepongeza hatua hiyo. Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmier, amesema anataraji kuwa hii ni ishara na kwamba Iran itazingatia kutafuta suluhu ya mizozo mingine inayo ikabili nchi hiyo kama vile mpango wake wa nyuklia.