1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tetemeko la pili katika siku mbili Japan

16 Aprili 2016

Kiasi watu13 wamefariki na zaidi ya 1,000 wamejeruhiwa katika tetemeko kubwa la pili la ardhi katika muda wa siku mbili ambalo limelikumba eneo la kusini mwa kisiwa cha Kyushu nchini Japan leo Jumamosi(16.04.2016).

https://p.dw.com/p/1IWrd
Japan Erneutes Erdbeben
Majengo yaliyoharibiwa na tetemeko la ardhi JapanPicha: Reuters/Kyodo

Watu wengine darzeni kadhaa wamenaswa ama kufunikwa na kifusi, na serikali ilitarajiwa kupeleka wanajeshi 20,000 katika eneo hilo lililoathirika, katibu mkuu wa baraza la mawaziri Yoshihide Suga ameuambia mkutano na waandishi habari.

Wanafunzi sita wa chuo kikuu wamenaswa katika jengo lililoanguka katika kijiji cha Minamiaso, limeripoti shirika la utangazaji la NHK.

Japan Erneutes Erdbeben
Maporomoko ya ardhi baada ya tetemeko la ardhi JapanPicha: Reuters/Kyodo

Tetemeko hilo la ardhi , ambalo hapo awali lilikadiriwa kufikia wastani wa 7.0 limeshambulia siku moja baada ya watu tisa kuuwawa na wengine 1,100 kujeruhiwa katika tetemeko lililokuwa katika kiwango cha 6.5 katika kipimo cha Richter katika eneo hilo hilo, ikiwa ni kubwa zaidi katika muda wa miaka mitano.

Tetemeko hilo lililotokea leo Jumamosi (16.04.2016)lilitokea majira ya alfajiri na kitovu chake kilikuwa katika wilaya ya Kumamoto katika kina cha kilometa 12, na lilifuatiwa na matetemeko mengine madogo madogo, limesema shirika la utabiri wa hali ya hewa.

Japan Erneutes Erdbeben
Kituo cha kuhifadhi watu baada ya tetemeko la ardhi nchini JapanPicha: Getty Images/T. Karibe

Uharibifu wa majengo

Uharibifu zaidi katika nyumba na majengo mengine umeripotiwa Jumamosi katika wilaya ya mji wa Mashiki, eneo lililoathirika zaidi na tetemeko hilo siku iliyopita, kilometa 900 kusini magharibi mwa Tokyo.

Picha za televisheni zinaonesha nyumba zilizoharibiwa, majengo yaliyoanguka, mipasuko barabarani na maporomoko makubwa ya ardhi katika kijiji cha Minamiaso, kilometa 20 mashariki mwa Mashiki.

Daraja lenye urefu wa mita 200 liliporomoka katika bonde na jengo la halmashauri ya jiji liliporomoka katika mji wa Uto, kusini magharibi mwa wilaya hiyo na kilometa 5 kutoka baharini.

Japan Erneutes Erdbeben
Waokoaji wakiwatafuta watu kutoka katika kifusi cha nyumba iliyoporomokaPicha: Getty Images/T. Karibe

Uwanja wa ndege wa Kumamoto , kilometa 15 kaskazini magharibi mwa Mashiki, ulifungwa baada ya dari kuanguka, shirika la utangazaji la NHK limeeleza.

Zaidi ya nyumba 200,000 zilikuwa hazina umeme katika kitongoji cha wilaya ya Kumamoto, Miyazaki na Oita, shirika la habari la Kyodo limeripoti.

Kumekuwa na mitetemeko zaidi ya 60 katika muda wa masaa tisa baada ya tetemeko hilo , taarifa hiyo imesema.

Japan Erneutes Erdbeben
Waokoaji wakimtoa mtoto kutoka katika nyumba iliyoporomokaPicha: Reuters/D. Wada/Mainichi Shimbun

Hatari zaidi

Gen Aoki , mkurugenzi wa idara inayoshughulika na matetemeko ya ardhi na tsunami katika idara ya utabiri wa hali ya hewa, amesema matetemeko ya siku iliyopita yanaonekana kuwa ni "matayarisho ya tetemeko kubwa zaidi" siku ya Jumamosi.

Matetemeko madogo madogo zaidi pamoja na kuporomoka kwa ardhi ni hatari huku kukitarajiwa mvua kubwa baadaye katika eneo hilo leo Jumamosi(16.04.2016), ameuambia mkutano na waandishi habari.

Japan Erdbeben in Kumamoto
Majengo yaliyoanguka baada ya tetemeko la ardhiPicha: Getty Images/AFP/K. Nogi

Hakuna kitu ambacho si cha kawaida katika vinu vitatu vya kinyuklia vya karibu, ikiwa ni pamoja na kituo cha umeme cha Sendai katika wilaya ya Kagoshima, Suga amewaambia waandishi habari.

Kinu cha umeme cha Sendai kiko kilometa 130 kusini mwa Kumamoto.

Kituo cha kuzalisha umeme cha Kyushu kilifungua vinu viwili vya kinyuklia mwaka jana, kikiwa kinu cha kwanza nchini humo chini ya sheria mpya za udhibiti.

Mwandishi: Sekione Kitojo / dpae

Mhariri: Isaac Gamba