1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump ampa kisogo Guaido, agusia kukutana na Maduro

Saumu Mwasimba
22 Juni 2020

Rais wa Marekani Donald Trump amesema atafikiria kukutana na rais wa Venezuela Nicolas Maduro na kuonesha ishara kwamba hana imani kikamilifu na kiongozi wa upinzani wa Venezuela Juan Guaido.

https://p.dw.com/p/3eA6u
Venezuela Juan Guaidó
Picha: Imago Images/Agencia EFE/R. Pena

Mahojiano yaliyochapishwa jumapili yamemnukuu rais huyo wa Marekani Donald Trump akisema atafikiria kukutana na Maduro.Na kwasababu Maduro angependa kukutana,yeye Trump hapingi mikutano. Hivvyo ndivyo alivyonukuliwa Trump. Lakini pia akaongeza kusema kwamba siku zote anasema hana cha kupoteza kwa kufanya mikutano ingawa kwahivi sasa mikutano kadhaa ameikataa.

Kauli hii ya Trump inatowa ishara kwamba hana imani kikamilifu na kiongozi wa upinzani wa nchi hiyo ya Venezuela Juan Guaido aliyejitangaza kuwa rais mnamo mwezi Januari mwaka 2019,wakati taifa hilo lilipotumbukia kwenye mapambano ya kuwania madaraka, kati ya kiongozi huyo wa upinzani na rais Maduro.

Mapambano hayo ya kuwania madaraka yalichochewa na matokeo ya uchaguzi uliosusiwa na upinzani na kukataliwa pia na Jumuiya ya Kimataifa uliodai ni wizi.

Venezuela: Proteste der Opposition in Caracas
Wafuasi wa kiongozi wa upinzani Juan GuaidoPicha: Getty Images/AFP/F. Parra

Takriban nchi 60 ikiwemo hiyo Marekani zilitangaza kumtambua Guaido ispokuwa China na Urusi zilizotoka wazi na kumuunga mkono rais Maduro ambaye utawala wake umeandamwa na vikwazo chungunzima kutoka Marekani.

Hata hivyo licha ya mivutano iliyopo rais wa Marekani Donald Trump ameuambia mtandao wa habari wa Axios kwamba angependa kuiacha wazi nafasi ya kukutana na Maduro.

Lakini pia tambua kwamba uhusiano kati ya serikali mjini Washington na ile Maduro,mjini Caracas ambayo ni ya kisoshalisti sio mzuri na hali ilizorota zaidi mwezi Mei baada ya Venezuela kuwakamata Watu 52 wanaodaiwa kuwa Mamluki ,miongoni mwao wakiwemo wanajeshi wawili wastaafu wa Marekani .

Venezuela imedai kwamba kundi hilo linapanga uvamizi wa kijeshi wa majini kwa msaada wa Marekani. Hata hivyo Marekani imekanusha kuhusika.

Venezuelas Präsident Nicolas Maduro
Rais wa Venezuela Nicolas Maduro Picha: picture-alliance/dpa/Prensa Miraflores/J. Zerpa

Lakini pia licha ya serikali ya Marekani kwa kipindi chote kumuunga mkono kiongozi wa upinzani wa Venezuela mtandao huo wa Axios uliomuhoji Trump umesema wakati wa mahojiano hayo Trump alionesha ishara ya kutokuwa na imani kubwa na Guaido akisema anapinga kinachoendelea Venezuela lakini kuhusu kumtambua Guaido ,anasema hakuona kosa lakini hafikiri kwamba ulikuwa uwamuzi wa maana kwa njia moja au nyingine.

Mahojiano hayo yamechapishwa wakati ikulu ya Marejani ikishughulikia kuibuka kwa madai katika kitabu kilichoandikwa na aliyekuwa mshauri wa masuala ya usalama wa taifa wa rais Trump,John Bolton,ambaye alikuwa mtu muhimu katika juhudi nyingi za kidiplomasia.

Kwa mujibu wa baadhi ya vifungu vya kitabu hicho vilivyochapihswa na mtandao wa Axios,Bolton aliandika kwamba mawazo ya Trump yalimuona Guaido kuwa mtu dhaifu kinyume na Maduro aliyekuwa na nguvu.

Hata hivyo katika mahojiano hayo ya Jana na Axios rais Trump alimkosoa Bolton akisema ni kiumbe wa mwisho asiyekuwa na akili duniani kwa kuunga mkono vita vya Iraq.