1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump sasa aitaka China iwachunguze Joe Biden na mwanawe

Zainab Aziz Mhariri: Grace Patricia Kabogo
4 Oktoba 2019

Licha ya Trump kukabiliwa na uchunguzi kuhusu kumshinikiza Rais wa Ukraine awachunguze aliyekuwa makamu wa Rais wa Marekani na mwanawe, sasa kiongozi huyo ametoa wito kwa China iwachunguze Joe Biden na Hunter Biden.

https://p.dw.com/p/3QhnT
USA Washington Weißes Haus | Präsident Donald Trump
Picha: picture-alliance/Zuma Press/White House

Rais wa Marekani Donald Trump ameitaka China wazi wazi iwachunguze aliyekuwa makamu wa rais wa Marekani, Joe Biden na mwanawe. Trump aliwaambia waandishi wa habari ikulu, kwamba China inapaswa kuanza uchunguzi huo licha ya Rais huyo kukabiliwa na kitisho cha kufanyiwa uchunguzi unaoweza kusababisha aondolewe madarakani. Uchunguzi huo dhidi ya Trump unatokana na madai kwamba alimshinikiza Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy amchunguze Biden na mwanawe Hunter Biden.

Mwenyekiti wa kamati ya upelelezi ya bunge la Marekani wa chama cha Democratic Adam Schiff amesema kauli za Trump zinaonyesha rais huyo anahisi kuwa anaweza kufanya anachotaka bila ya kuwajibishwa. Schiff amesema tabia hiyo ni hatari kwa usalama wa taifa.

Mwenyekiti wa kamati ya upelelezi ya bunge la Marekani wa chama cha Democratic Adam Schiff
Mwenyekiti wa kamati ya upelelezi ya bunge la Marekani wa chama cha Democratic Adam SchiffPicha: picture-alliance/AP Photo/P. Monsivais

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Marekani, Ellen Weintraub amesema hatua za Trump ni ukiukaji wa sheria kuhusu matumizi ya fedha za kampeni kwa mtu yeyote anayeomba au kupokea kitu chochote cha thamani kutoka kwenye taifa la nje kuhusiana na uchaguzi wa Marekani. Joe Biden ni miongoni mwa wanachama wa chama cha Democratic wanaotarajia kumpinga Trump katika uchaguzi wa mwaka ujao wa 2020.

Hapo awali Rais Trump alikanusha taarifa kwamba aliishinikiza serikali ya kigeni kuchukua hatua dhidi ya mpinzani wake kwa manufaa yake binafsi na pia kuingilia kati siasa za ndani. Maoni ya hivi karibuni yanapendekeza kuwa Trump anajaribu kuifanya tabia hiyo ionekane kuwa ni jambo la kawaida. Maoni hayo pia yanakumbusha wito wake wa mwaka 2016 kwa Urusi alipoitaka ichapishe mawasiliano ya barua pepe ya Hillary Clinton ambayo hata hivyo yalidukuliwa na kuchapishwa.

Trump na washirika wake mnamo wiki iliyopita walijaribu kuibua tuhuma dhidi ya shughuli za Biden na mwanawe huko nchini Ukraine. kwa mujibu wa chama cha Demeocratic, hili ni jaribio la dhahiri la kutaka kuitumbukiza familia hiyo kweye mashaka na ukosoaji mkubwa.

Mwanazuoni wa Marekani Allan Lichtman, aliyetabiri ushindi wa Donald Trump katika uchaguzi wa Rais wa mwaka 2016 katika mahojiano ya mweezi Desemba mwaka jana na DW, alitabiri kwamba Rais huyo wa Marekani ataodolewa madarakani mwaka huu wa 2019.

Chanzo:/ https://p.dw.com/p/3QhOP