1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Twitter yaondoa alama ya buluu kwa akaunti za watu mashuhuri

Mohammed Khelef
21 Aprili 2023

Mtandao wa kijamii wa Twitter umeanza zoezi kubwa la kuondoa Tiki ya Bluu ambazo zilikuwa zikitumika kuthibitisha utambulisho wa watu mashuhuri.

https://p.dw.com/p/4QPcq
Twitter Logo
Picha: CONSTANZA HEVIA/AFP

Mabadiliko hayo yamefanyika baada ya mmiliki wa Twitter, Elon Musk, kuanzisha huduma ya malipo ya kila mwezi ili kuipata alama ya buluu mwaka jana.

Vyombo vingi vikubwa vya habari duniani kuanzia katika mataifa ya Ulaya, Urusi, China na nchi nyinginezo, vimepoteza alama hiyo ya buluu kuanzia Alhamis (Aprili 21).

Akaunti nyingi pia za watu maarufu katika mtandao wa Twitter, akiwemo kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis, mwimbaji nyota wa Marekani Beyonce, mtangazaji mashuhuri Oprah Winfrey, rais wa zamani wa Marekani Donald Trump na msanii wa muziki  Lady Gaga nazo pia ziliondolewa utambulisho huo.

Takribani watumiaji 300,000 walikuwa na alama hiyo ya buluu kabla ya Musk kutangaza kuwa na malipo ya kila mwezi.

Uamuzi huo umezusha wasiwasi juu ya kuenea kwa habari za uongo kupitia akaunti bandia.