1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi wa Ivory Coast, raundi ya pili inanukia!

Abdu Said Mtullya3 Novemba 2010

Huenda ikafanyika raundi ya pili ya uchaguzi nchini Ivory Coast.

https://p.dw.com/p/PxZd
Rais wa Ivory Coast Laurent Gbagbo akipiga kura.Picha: AP

Nusu ya kura zimeshahesabiwa katika uchaguzi wa urais nchini Ivory Coast na rais Laurent Gbagbo yupo mbele ya mpinzani wake Alassane Quattara kwa kura chache sana.

Shirika la habari la AFP limeripoti kwamba rais aliyepo madarakani Laurent Gbagbo mpaka sasa ameshapata asilimia 37 ya kura wakati mpinzani wake Alassane Quattara amefikia asilimia 34 ya kura baada ya nusu ya kura kuhesabiwa.

Matokeo hayo ya hadi sasa yanaashiria uwezekano wa kufanyika raundi ya pili ya uchaguzi.Msemaji wa tume ya uchaguzi Bamba Yacouba alitangaza mapema asubuhi leo kwa njia ya televisheni baada ya nusu ya kura milioni 4.5 kuhesabiwa.Kwa mujibu wa hesabu hizo zilizopatikana, aliekuwa rais hapo awali Henri Konan Bedie yupo katika nafasi ya tatu akiwa amefikia asilimia 27.

Uchaguzi huo umefanyika baada ya kusubiriwa kwa muda mrefu sana.Watu wa nchi hiyo ya Afrika magharibi Ivory Coast wameupokea vizuri uamuzi wa kufanyika uchaguzi huo na asilimia 80 ya wastahiki walijitokeza na kupiga kura .

Tume huru ya uchaguzi imepaswa kisheria kutangaza sehemu ya matokeo ya kura zilizopigwa jumapili iliyopita.Lengo la uchaguzi huo unaofanyika baada ya kuahirishwa mara sita ni kuleta umoja wa nchi baada ya sehemu ya kaskazini kuwa chini ya udhibiti wa waasi kwa muda wa miaka mingi.

Mwandishi/Mtullya Abdu/ AFPE/Adeye,Julien/DW-Afrika/Französich/

Mhariri/Josephat Charo/